NA MATUKIO DAIMA MEDIA
Maafisa 11 wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Kanda ya Mashariki leo wamepandishwa vyeo baada ya kupitia kozi mbalimbali zinazotolewa na Jeshi hilo na kuhitimu.
Aidha upandishwaji wa vyeo kwa maofisa hao umetokana na taratibu zilizofanyika na kupimwa utendaji wao wa kazi hadi wakafikia hatua ya kuwapandisha vyeo.
Akizungumza Jijini Dar es salaam na waandishi wa habari baada ya zoezi la uvalishaji vyeo kwa maafisa hao kwa niaba ya Kamishna Jenerali wa Zimamoto na Uokoaji Nchini, Naibu Kamishna wa Jeshi hilo,DCF Kennedy Komba amewasihi maafisa hao kufanya kazi kwa weledi na kumtanguliza mwenyezi Mungu kwenye majukumu yao.
"Leo tulikua na zoezi la uvalishaji vyeo kwa maafisa wa ngazi mbalimbali ambao kwa mujibu wa taratibu za Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mheshimiwa Rais imempendeza awapandishe vyeo." amesema DCF Komba
Amesema kuwa,zoezi hilo lilipaswa kufanywa na Kamishna Jenerali wa Jeshi hilo lakini amekaimishwa kufanya hivyo kwa niaba yake nakwamba baadhi ya maafisa waliyopatiwa vyeo ni kutoka ngazi ya Kamishna msaidizi(Assistance Commissioner) mpaka mkaguzi wa Zimamoto na Uokoaji.
"Kwa niaba ya Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji namshukuru Mh. Rais kwa kutoa kibali cha upandishwaji vyeo kwa maafisa hawa,kwani naamini katika kupandishwa kwao vyeo kwanza watakua wameongeza ari ya kufanya kazi,
Sambamba na hilo, wataenda kutimiza majukumu mengine kwa sababu unapopandishwa cheo kama askari ndio unaongezewa majukumu mengine ya kusimamia wafuasi na kufanya kazi za ziada zaidi,hivyo wanaenda kuleta tija katika kutoa huduma ya kuzima moto na kuokoa maisha ya watu na Mali zao."amesema
Ameongeza anaishukuru Wizara ya mambo ya ndani kwa kuona umuhimu wa hao maafisa kupandishwa vyeo sababu jambo hilo lina mchakato hadi inapofikia mtu anapandishwa cheo, anaamini Waziri na Menejimenti yake ya Wizara ikawapendeza hawa ambao wapo katika Mikoa ya kanda hii ya Mashariki ambayo imejumuisha Mikoa ya Lindi,Pwani na Dar es salaam."
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo Cha Uchunguzi Mkoa wa Kizima Moto Ilala Dar es salaam ambaye amepandishwa cheo na kuwa Kamishna Msaidizi wa Jeshi hilo Tanzania Bara ACF Chrispin Jackson Rabiuzima, amesema kuwa maafisa waliopandishwa vyeo ni kutoka kamandi tano ambazo ni kamandi ya Zimamoto Temeke,Ilala,Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere,Kinondoni,Mkoa wa Pwani,pamoja na maafisa kutoka Mkoa wa Morogoro,na kamandi ya Mkoa wa Lindi.
"Leo ni siku ya furaha kwangu namshuku Mwenyezi Mungu nimeipokea taarifa hii kwa muda muafaka,nahidi kufanya kazi kwa bidii na uweledi wa hali ya juu.
Ameongeza "Namshukuru Rais wa Jumhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan,pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi bila kumsahau Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zima moto na Uokoaji kwa kuona tunastahili kupanda cheo kwa wakati huu,tumepokea kwa moyo mkunjufu na moyo mnyenyekevu,tuna ahidi kuchapa kazi" amesema.
Aidha ACF Rabiuzima amebainisha kuwa maafisa na askari hao 11 waliopandishwa vyeo hivyo na idadi yao kwenye mabano kuwa ni kutoka cheo cha Mrakibu Mwandamizi kuwa Kamishna Msaidizi(2),Mrakibu kuwa Mrakibu Mwandamizi(4),Mrakibu Msaidizi kuwa Mrakibu(3), na Mkaguzi Msaidizi kuwa Mkaguzi(2).
0 Comments