Na Fadhili Abdallah,Kigoma
UPIGAJI kura katika uchaguzi mdogo wa udiwani kata ya Kasingirima Manispaa ya Kigoma Ujiji unaendelea huku ikielezwa hali ya amani na usalama ikitawala zoezi zima licha ya kuwepo kwa idadi ndogo ya watu wanaojitokeza kupiga kura.
Msimamizi wa uchaguzi huo,Mwantumu Mgonja akizungumza na waandishi wa Habari kwenye ofisi ya Mtendaji kata ya Kasingirima ambapo zoezi la kuhesabu na kufanya majumlisho ya kura litafanyika alisema kuwa hadi sasa hakuna changamoto yeyote iliyojitokeza na kwamba wanaamini uchaguzi utaisha salama.
Mgonja alisema kuwa vyama 12 vimeweka wagombea kwenye uchaguzi huo huku kukiwa na jumla ya watu 1964 wanaotarajia kupiga kura katika vituo sita vilivyoteuliwa kwa ajili ya zoezi hilo.
Mgombea wa CCM katika uchaguzi huo,Mlekwa Kigeni alisema kuwa hadi sasa hajasikia kuwepo kwa changamoto kwenye zoezi hilo la uchaguzi na anaamini kwamba kwa jinsi lilivyoanza litaisha vizuri licha ya idadi ndogo iliyojitokeza asubuhi kwa sababu ya mvua kubwa lakini kufikia mchana huu idadi ya watu imeanza kuongezeka.
Kwa upande wake Katibu Mipango na uchaguzi ACT mkoa Kigoma,Issa Hussein alisema kuwa uchaguzi unaenda vizuri tangu ulipoanza lakini zipo changamoto ndogo ndogo za madiwani wa CCM kugawa fedha na uwepo wa watu wenye mabegi wa CCM wanaozunguka maeneo ya vituo ambao wanadhaniwa kuwa na kura ili waziingize kwenye vituo.
Mwisho.
0 Comments