Mkufunzi wa somo la Kilimo Cha Parachichi Aidan Kiwale akiwaonesha aina ya Parachichi washiriki wa mafunzo
NA MATUKIO DAIMA APP
VIJANA Mradi wa Youth Angecy Mufindi (YAM) wenye Ndoto ya kuwekeza kwenye Kilimo Cha zao la Parachichi wilayani Mufindi mkoa Iringa wamesema kutokana na mwamko mkubwa wa wananchi wengi kuwekeza katika kilimo cha zao hilo kuna uwezekano mkubwa wa soko la Parachichi kuendelea kuporomoka zaidi iwapo serikali haitachukua hatua kutafuta wawekezaji wa viwanda vya kuchakata Parachichi ama serikali yenyewe kujenga kiwanda chake .
Kuwa hadi sasa bei ya Parachichi kwa kilo moja imeshuka kutoka kiasi cha shilingi 18000 hadi kufikia kiasi cha shilingi 1500 kwa kilo hali ambayo ni hatari zaidi kwa mkulima wa zao hilo la Parachichi kupata faida kwa kilimo hicho .
Akizungumza wakati wa mafunzo ya Kilimo kwa vijana wa mradi wa Youth Angency Mufindi (YAM) Leo katika ukumbi wa Yatima Igoda kata ya Luhunga mkufunzi wa mafunzo hayo Aidan Kiwale alisema awali wakulima wa zao la Parachichi walikuwa wakitegemea zaidi kilimo hicho kuliko mazao mengine ya biashara kutokana na kuwa na soko la uhakika na wanunuzi walikuwa wakifika hadi shambani ila sasa imekuwa tofauti hasa upande wa bei .
Kwani alisema msimu wa mavuno ya Parachichi ndio kwanza umeanza hivyo walitegemea mwanzo wa mavuno bei kuwa nzuri zaidi ila matokeo yake wameanza na mwanzo mbaya kwani kilo ni Tsh 1500 tofauti na mwaka jana walipouza kilo moja hadi kiasi cha shilingi 1800 na maeneo mengine waliuza hadi shilingi 2000.
Hivyo alisema imani kubwa kwa wakulima wa zao hilo ipo mikononi mwa serikali kupitia wizara ya viwanda kuona inawatafuta wawekezaji zaidi watakaofanya uwekezaji katika sekta ya mazao ya matunda hayo ya Parachichi ili kumwezesha mkulima kupata faida kama ilivyo maeneo mengine ambayo yafanya vizuri katika uzalishaji wa mazao ya biashara .
Kiwale alisema pamoja na kilimo cha Parachichi kwa wilaya ya Mufindi kuendelea kushika kasi kwa kila mwananchi kutamani kuwekeza katika kilimo hicho ila wasiwasi wao ni kuendelea kupata soko la uhakika la zao hilo .
" Imani yetu kubwa kwa mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kama alivyofanya jitihada kubwa ya kutujengea barabara ya lami kutoka Sawala hadi Iyegea na kutufanya wakulima kusafirisha mazao yetu kwa urahisi zaidi tunategemea kilio chetu cha kiwanda cha kuchakata zao la Parachichi kikajengwa katika mkoa wetu ili kumkomboa mkulima " alisema Kiwale
Kuwa nguvu kubwa imefanywa na mradi wa YAM kuwapatia elimu vijana toka familia zenye mazingira magumu na mwitikio wa vijana hao kuwekeza katika kilimo cha Parachichi ni mkubwa zaidi hasa kutokana na faida kubwa iliyopo katika kilimo hicho ukilinganisha na kilimo cha mazao ya mengine kama mahindi na nyanya .
Kwani alisema mti mmoja wa Parachichi iwapo utatunzwa vizuri unaweza na kulimwa kwa kitaalamu kwa kipimo cha mita 10 kwa 10 katika eka mmoja utakuwa na mita 40 baada ya miaka mitatu kwa baadhi ya mbegu utakuwa na wastani wa matunda 1000 kwa miti 10 pekee hivyo kwa miti 40 utakuwa na jumla ya matunda 40,000 na mti huo huo mmoja ukifika baada ya miaka minne ama mitano unaweza kutoa matunda 1200 na hivyo kuwa na uhakika wa kupata milioni 1 kwa miti 10 kwa mwaka mzima tofauti na mkulima wa zao la Mahindi .
" Leo wewe mkulima wa Parachichi ukiuza unaweza kwenda kununua mahindi utapata madebe 150 kwa kuuza matunda yako miti 10 pekee hivyo zao hilo linalipa japo linaweza kulipa zaidi kama bei elekezi ya serikali ikatolewa "
Tofauti na mazao mengine zao hilo la Parachichi ni zao lenye faida kuwa iwapo kama kutakuwa na soko la uhakika na kuwa na bei elekezi ya serikali katika zao hilo isiwe mfanyabiashara analipa kwa kujisikia yeye na sio matakwa ya mkulima .
Washiriki wa mafunzo hayo Ester Kahama kutoka kata ya Ihanu alisema elimu aliyopata ya kilimo cha Parachichi itapelekea kuongeza ufanisi zaidi tofauti na kilimo cha mazoea ambacho alikuwa akilima awali .
Japo alisema Kasi ya Wakulima itashusha bei ya zao hilo hivyo ni vema mazingira ya uhamasishaji Kilimo Cha Parachichi yaende na uhamasishaji wa uanzishwaji viwanda vya kuongeza thamani ya zao hilo.
Alisema kupitia mradi huo wa YAM ameweza kupata elimu ya kutosha ya kilimo bora cha Parachichi na kuwa hivyo si tu atakwenda kuongeza kasi ya uzalishaji bali atakuwa mwalimu mzuri kwa wananchi wa kijiji na kata anayotoka .
Huku kijana Nehemia Mkusi kutoka kijiji cha Ispii Ihanu alisema wamejifunza faida ya kilimo cha Parachichi pamoja namna ambavyo kilimo hicho kinavyoweza kumkomboa kijana .
Mafunzo hayo ya kilimo na ujasiriamali kwa vijana yameendelea kutolewa na Halmashauri ya wilaya ya Mufindi Mufindi chini ya mradi wa Foxes Community and Wildlife Conservation( FCWC) na YAM kupitia ufadhili wa Finland mradi unaotekelezwa kwenye kata za Mdabulo ,Luhunga na Ihanu katika wilaya ya Mufindi huku lengo la mradi lilikuwa kuwafikia vijana 320 ila hadi sasa toka mradi ulipoanza mwaka 2021 tayari wanufaika 420 kwa vijiji vyote 16 wamefikiwa .
0 Comments