Na Hamida Ramadhan Dodoma
KATIBU Mkuu Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dkt Jim Yonaz amesema kuwa zaidi ya watu milioni 18 duniani wamekuwa wakitumia huduma ya mtandao (internet) idadi ambayo ni kubwa hivyo ni muhimu kuweka namna sahihi ya kulinda usalama wa watumiaji hao.
Pia amesema Serikali itaendelea kuwalinda wananchi wake kutokana na uhalifu wa mitandao ili kuhakikisha nchi inakuwa salama.
Hayo amebainisha leo na katibu mkuu huyo wakati akifunga mafunzo ya siku tano yanayohusu usalama mtandaoni kwa wapelelezi na Askari wa chumba cha Mashtaka jijini Dodoma.
" Jambo la usalama mtandao ni muhimu kutiliwa mkazo hasa katika zama hizi za kidigitali kwa kuwa uwepo wa usalama katika matumizi ya mitandano ni sawa sawa na kuhakikishia dunia inakuwa salama," amesema Katibu Mkuu huyo
Na kuongeza kusema "Dunia sasa imebadilika tofauti na ilivyokuwa zamani,hivi sasa masuala ya usalama na ulinzi yanategemea TEHAMA,wachafuzi nao wanapata fursa kuharibu kutumia Teknolojia hiyo kuvuruga amani,nawaomba mkaendelee kuboresha mbinu mlizojifunza hapa kuhakikisha usalama katika matumizi ya mitandao unaboreshwa,hakikisheni mnaepusha madhara ya matumizi mabovu ya mitandao,” amesema Dkt. Yonaz.
Amesema, kupitia mafunzo hayo ya siku tano,walinzi hao wa usalama mtandaoni wanapaswa kushirikiana katika hatua changamoto zote uhalifu mtandao na kwamba Kwa kufanya hivyo watadhihirisha namna ambavyo Tanzania imejipanga katika kuhakikisha matumizi ya mitandao yanakuwa salama.
"Tunaamini kuwa tunayo nchi inayojilinda ,tunao wananchi wanaotegemea sana ulinzi wa mtandao Ili waishi Kwa amani na kuendelea kufanya shughuli nyingine za uzalishaji bila woga,ni jukumu lenu kulinda usalama wa taifa hili kwa kuzuia uhalifu wowote wa mtandao,"amesema
Naye, Mkurugenzi wa Mashtaka nchini(DCI)Camilius Wambura idara hiyo itahakikisha inaboresha mifumo ya kuhakiki uhalali wa taarifa zinazopitia kwenye mitandao ambayo imebuniwa na wataalam wa Teknolojia ya Habari nchini Ili kuzuia matumizi mabaya ya mitandao.
"Makosa ya mtandao yanakuwa mengi na kusababisha uvunjifu wa amani na kuharibu furaha Kwa watu wengine,kupitia mafunzo hayo yataleta matokeo chanya kutokana na mbinu mlizopata ili kukabiliana na uhalifu wa kimtandao kwani maarifa yatawasaidia katika kubadilishana taarifa,"Amesema.
Kadhalika Wambura ametumia nafasi hiyo kuwataka wapelelezi hao pamoja na askari kuhakikisha wanazingatia misingi ya kazi na wito wa maadili ya kazi yao ikiwa ni pamoja na kufanya kazi kwa kushirikiana ili kuweza kufikia malengo.
"Nendeni mkahakikishe mnafanya kazi kwa uadilifu na nidhamu katika utendaji kazi wenu kwani tabia za wachache zimekuwa zikiharibu taswira ya Jeshi jambo ambalo si jema,"amesisitiza.
0 Comments