Mshambuliaji wa Manchester City Raheem Sterling anasema kwamba atakuwa tayari kuondoka katika klabu hiyo iwapo hatopatiwa muda mwingi wa kucheza katika uwanja wa Etihad.
Mchezaji huyo wa England , ambaye kandarasi yake inakamilika 2023, amesema kwamba alikuwa na ndoto ya kucheza ughaibuni tangu akiwa mdogo.
‘’Iwapo kungekuwa na fursa kwenda kwengine, ningekuwa tayari kufanya hivyo’’, alisema Sterling mwenye umri wa miaka 26.
‘’Kwa sasa soka ndicho kitu muhimu kwangu. Nimekuwa na malengo ya kucheza ughaibuni ili kupata changamoto mpya’’.
Sterling alianzishwa katika mechi moja ya ligi ya Premia tangu ligi ya England kuanza, ijapokuwa alishiriki katika katika kikosi cha kwanza cha kombe la klabu bingwa Ulaya kilichoshindwa na PSG tarehe 28 Septemba.
Kuwasili kwa mchezaji mwenza wa England Jack Grealish kutoka Aston Villa kwa dau la £100m kumeongeza ushindani kwa nafasi za washambuliaji katika klabu ya City ijapokuwa kutokuwepo kwa Ferran Torres kwa takriban mwezi mmoja baada ya kupata jeraha la mguu kumepunguza chaguo la Guardiola.
Sterling alijiunga na City kutoka Liverpool mwaka 2015, na amefanikiwa kushinda mataji matatu ya ligi ya England, kombe la FA na kushinda taji la Carabao mara nne.
Chanzo; BBC Swahili.
0 Comments