Na Hamida Ramadhan, Matukio Daima Media Dodoma
SERIKALI inaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya utafutaji wa mafuta na gesi katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuimarisha sekta ya nishati na kuongeza mchango wake katika ukuaji wa uchumi wa taifa.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA), Mhandisi Charles Sangweni, amesema shughuli za utafutaji zinaendelea katika maeneo mbalimbali ikiwemo Eyasi-Wembere pamoja na vitalu vya Lindi na Mtwara vinavyotekelezwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).
Akizungumza na waandishi wa habari katika Wiki ya Utumishi wa Umma iliyohitimishwa jijini Dodoma, Mhandisi Sangweni amesema Tanzania imeendelea kuweka mkazo katika usimamizi wa rasilimali za petroli ili kuhakikisha zinatumika kwa manufaa ya taifa na wananchi.
Amesema pamoja na juhudi zilizofanyika kwa miaka mingi katika kutafuta mafuta, mafanikio makubwa yamepatikana kupitia ugunduzi wa akiba kubwa ya gesi asilia ambayo imeendelea kuwa nguzo muhimu katika maendeleo ya sekta ya nishati nchini.
“Tanzania imebahatika kuwa na akiba kubwa ya gesi asilia ambayo imefungua fursa mbalimbali za uwekezaji, ajira na maendeleo ya viwanda. Hii ni rasilimali muhimu ambayo tunapaswa kuitumia kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” amesema Sangweni.
Ameeleza kuwa mahitaji ya gesi asilia yanaendelea kuongezeka katika soko la dunia kutokana na jitihada za mataifa mbalimbali kutumia nishati safi zaidi, hali inayoongeza umuhimu wa rasilimali hiyo katika maendeleo ya kiuchumi.
Kwa mujibu wake, Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, jambo ambalo limeongeza mahitaji ya gesi na kufungua fursa zaidi za uwekezaji katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta hiyo.
Sangweni amesema PURA inaendelea kusimamia utekelezaji wa sera ya ushirikishwaji wa wazawa (Local Content) ili kuhakikisha Watanzania wananufaika na shughuli za mafuta na gesi kupitia ajira, utoaji wa huduma na ushiriki katika miradi mbalimbali.
Aidha, amesema mamlaka hiyo imeweka mifumo ya kuwawezesha wataalamu wa Kitanzania kushiriki kikamilifu katika sekta hiyo kwa kuwaunganisha na wawekezaji wanaotekeleza miradi ya mafuta na gesi nchini.
Amesisitiza kuwa matumizi bora ya rasilimali za gesi asilia yanaweza kuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya kiuchumi, ukuaji wa viwanda na kuimarisha usalama wa nishati nchini.






0 Comments