Tanzania imeendelea kunadi vivutio vya utalii, mazao ya utalii na fursa za uwekezaji zinazopatikana nchini Tanzania katika onesho la Kimataifa la Utalii - OTM ( Outbound Travel Mart) linaloendelea, jijini Mumbai nchini India, ambalo limeanza rasmi tarehe 05 Februari,2026 na kuhitimishwa leo Februari 07, 2026.
Onesho la OTM ni jukwaa muhimu kimataifa katika kutangaza, kuendeleza na kukuza biashara za utalii duniani.
Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) ni miongoni mwa Taasisi zinazoshiriki onesho hili adhimu linalokutanisha wadau wakubwa wa utalii duniani na kuendelea kuonesha vivutio vya kipekee vya utalii vikiwemo wanyamapori, mandhari, fukwe, malikale na utamaduni sambamba na kuhamasisha fursa mbalimbali za uwekezaji zinazopatikana katika Hifadhi za Taifa ishirini na moja (21) zilizopo Tanzania.
Aidha, TANAPA inatumia jukwaa hili adhimu la onesho la OTM, kuendeleza mikakati ya nchi ya kujitangaza na kuongeza mashirikiano katika masoko ya utalii duniani. Hatua hii ni mkakati mahususi katika kuongeza idadi ya watalii wa kimataifa hususani soko la India wanaotembelea Hifadhi za Taifa Tanzania pamoja na kukuza pato la utalii na kuchangia kwa kiwango kikubwa uhifadhi na uchumi endelevu wa taifa kwa ujumla.
Ushiriki wa TANAPA katika onesho hili ni utekelezaji wa azma ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuvutia masoko mapya ya watalii, na kuendeleza utalii endelevu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.







0 Comments