Na Mariam Kagenda Kagera
Wadau wa maendeleo wilayani Muleba mkoani Kagera wamehimizwa kushirikiana na Serikali kuwasaidia watoto wenye mahitaji maalum ili waweze kuishi kama watoto wengine
Katibu Tawala wilaya ya Muleba Benjamini Mwikasyege amesema hayo wakati wa hafla fupi ya kukabidhi msaada wa vifaa vya shule kwa watoto wenye mahitaji maalum ambapo msaada huo umetolewa na Wenfurebe Foundation katika shule ya msingi Kaigara .
Bwana Mwikasyege amesema kuwa wapo watoto wengi wenye mahitaji maalum hivyo ni jukumu la wadau wa maendeleo kusaidiana na serikali kuwasaidia watoto hao na watu wengine wenye uhitaji .
Ameongeza kwa kuishukuru familia ya Wenfurebe kupitia Wenfurebe foundation kwa kuona umuhimu wa kuwasaidia watoto hao kwani wapo watu wengi wana fedha lakini hawajafanya jambo kama hilo.
Kwa upande wake mkurugenzi wa Taasisi ya Wenfurebe Foundation Adv Saimon Wenfurebe amesema kuwa Taasisi hiyo imetoa msaada wa vifaa vya shule kwa watoto 500 wenye mahitaji maalum .
Amesema kuwa Taasisi hiyo itaendelea kuwagusa watu wenye mahitaji maalum wakiwemo watoto kwani inatambua kuwa serikali haiwezi kubeba jukumu hilo peke yake isipokuwa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali .
Kwa upande wao baadhi ya wazazi wa watoto wenye mahitaji maalum waliopatiwa msaada wa vifaa vya shule pamoja na mahitaji mengine ya nyumbani wameishukuru Taasisi ya Wenfurebe kwa kuona umuhimu wa kuwasidia watoto hao kwani wanahitaji kupata mahitaji muhimu kama walivyo watoto wengine .








0 Comments