Serikali imetoa hati za hakimiliki za kimila 580 kwa wananchi wa Kijiji cha Makibo, Kata ya Nyahua, Wilaya ya Sikonge mkoani Tabora kupitia Mradi wa Usimamizi Shirikishi wa Misitu ya Miombo (DSL-IP), unaoratibiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), ili kuimarisha usalama wa milki za ardhi na kupunguza migogoro kati ya jamii na mamlaka za uhifadhi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa zoezi hilo jana, Mkuu wa Wilaya ya Sikonge, Mhe. Thomas Myinga, alisema hati hizo zitawawezesha wananchi kuwekeza katika shughuli endelevu za kilimo, ufugaji na biashara za mazao ya misitu, hatua itakayochochea uchumi wa kaya na kulinda mazingira.
“Mipango hii na hati hizi ni nyenzo muhimu katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, kupunguza upotevu wa bioanuwai na uharibifu wa ardhi. Tunataka kuona jamii zikiwekeza katika matumizi bora ya ardhi na uhifadhi wa misitu ya miombo,” alisema Myinga.
Kwa upande wake, Kaimu Naibu Kamishna wa Uhifadhi wa TFS, Dkt. Zainab Bungwa, alisema mradi huo wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 6.8 (sawa na Sh bilioni 16.8) unatekelezwa kwa miaka mitano (2023–2027) katika wilaya za Kaliua, Urambo na Sikonge (Tabora) na Mlele (Katavi) kwa lengo la kurejesha uoto wa asili, kupunguza uharibifu wa ardhi na kuboresha maisha ya wananchi.
Amesema mradi huo unahusisha nchi 11 ikiwamo Tanzania, Kenya, Malawi, Zimbabwe na Angola, na umeanza kwa kutambua vikundi vya wazalishaji wa misitu na mashamba (FFPOs) ili kuviwezesha kushiriki katika shughuli za uhifadhi na biashara endelevu.
Dkt. Bungwa aliongeza kuwa TFS inatekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa vituo vya ulinzi wa misitu (Ranger Posts), matumizi ya ndege zisizo na rubani (drones) kwa ulinzi, ujenzi wa nyumba za nyuki, maghala ya mbegu na miundombinu ya maji kwa ajili ya jamii zinazoshiriki uhifadhi.
Kwa upande wake, Obed Katonge kutoka Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi alisema tume itaendelea kushirikiana na mamlaka za upangaji ili kuhakikisha ardhi inapangwa, kupimwa na kumilikishwa kwa wananchi, huku akisisitiza wananchi kulinda hati zao na kuepuka kuazimishana, kwani kufanya hivyo ni kuvunja sheria.

















0 Comments