Awashukuru kwa kutoa fursa ya Ushiriki wa upigaji Kura Oktoba 29_
_Sherehe hizo kuhusisha Tohara kwa Kundi rika la Vijana zaidi ya 2, 000_
Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla leo Jumatatu Oktoba 20, 2025, amezindua sherehe za msimu wa tohara kwa jamii ya Kimasai nchini Tanzania, akiishukuru Jamii hiyo kwa kuheshimu sheria na Miongozo ya nchi kwa kusimamisha shughuli za Tohara Oktoba 29, 2025 ili kuruhusu Makundi rika mbalimbali kwenda kupiga kura kuwachagua Viongozi wanaowataka kuwaongoza kwa miaka mitano ijayo.
Sherehe hizo maarufu kama Enkipaata zimezinduliwa kwenye Kijiji cha Oldonyosapuk Wilaya ya Arumeru zikitarajiwa kuhusisha zaidi ya Vijana 2,000 wa kundi rika la Irmegoliki litakalodumu mpaka Oktoba 2032, akiwahakikishia usalama na amani wakati wote kuanzia sasa, siku ya upigaji wa kura na baada ya upigaji kura pamoja na kuwahimiza wananchi wote kushiriki kuchagua Viongozi wanaowataka katika uchaguzi huo.
"Ninawashukuru kwanza kwa kunipa heshima ya kuzindua sherehe hizi na zaidi ni kwamba pamoja na kuwa na mila zenu bado mmeheshimu taratibu na ratiba nyingine za serikali niwaombe tarehe 29 Viongozi wote mpaze sauti katika maeneo yote watu wapate haki ya kupiga kura na sisi kama Serikali tuwahakikishie kuwa uchaguzi utakuwa salama na wenye amani." Amesema Mhe. Makalla.
Kwa upande wake Kiongozi Mkuu wa Jamii ya Kimasai Isack Meijo Ole Kisongo na Mlezi wa kundi rika hilo linaloingia kwenye msimu wa tohara wamesema sababu ya kuiheshimu Oktoba 29, 2025 ni kutokana na Jamii hiyo kutambua umuhimu wa upigaji wa kura, wakiahidi kuwa Jamii kinara katika kumpa kura nyingi zaidi Mgombea wa nafasi ya Urais Dkt. Samia Suluhu Hassan kutokana na mapenzi yao kwake na maendeleo mengi aliyowatendea jamii ya Kimasai nchini katika sekta ya jamii na ufugaji.
0 Comments