Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania Bw. Gerson Msigwa amewahakikishia Watanzania wote wenye sifa na waliojiandikisha kwenye daftari na mpiga kura kuwa serikali ya awamu ya sita inatambua kikamilifu wajibu wake wa kulinda haki ya kila Mtanzania ikiwemo haki ya Kikatiba ya Kuchagua na kuchaguliwa, akiwahimiza kujitokeza kwa wingi kupiga kura ifikapo Oktoba 29, 2025.
Msemaji huyo wa serikali amewatoa hofu pia Watanzania dhidi ya yale yanayosemwa mtandaoni kuelekea siku ya uchaguzi Mkuu wa Tanzania, akisema serikali na Vyombo vya Dola vimejipanga na kujiandaa kikamilifu kuhakikisha kuwa uchaguzi unafanyika kwa amani na katika mazingira tulivu na salama ili kutoa fursa ya kila mmoja kuitumia haki yake ya Kikatiba.
"Naomba niwahakikishie Watanzania wote kuwa amani ipo tena ya kutosha kwahiyo msiwe na wasiwasi wowote serikali hii ni makini, Vyombo vyetu vyote vya Dola vimejiandaa kikamilifu kuhakikisha utulivu na amani ya kutosha. Nenda kachague Kiongozi unayemtaka na hakuna mtu yoyote atakayefanya chochote. Achaneni na maneno yanayotengenezwa mtandaoni kuwatishia watu na kuwaaminisha vitu ambavyo havitatokea." Amesema Msigwa.
Aidha Msigwa pia amehimiza watanzania kuendelea kujiandaa na upigaji huo wa kura kwa kusikiliza mikutano ya Kampeni ya Wagombea Udiwani, Ubunge na Urais wa Tanzania ili kuwa na maamuzi sahihi ya kuchagua Kiongozi anayefaa badala ya kusubiri kuchaguliwa Kiongozi wa eneo lako na watu wengine.
0 Comments