Kutiwa saini kwa makubaliano hayo siku ya Ijumaa kunafuatia "tamko la kanuni" ambalo lilikubaliwa mwezi Aprili
Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo zimetia saini mkataba wa amani mjini Washington unaolenga kumaliza miongo kadhaa ya mzozo mbaya kati ya majirani hao wawili, na uwezekano wa kuipatia Marekani upatikanaji wa madini yenye faida kubwa.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio aliwakaribisha mawaziri wa mambo ya nje wa nchi hizo mbili katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Washington kwa ajili ya kutia saini makubaliano hayo.
"Leo, ghasia na uharibifu unamalizika, na eneo lote linaanza kuwa na sura mpya ya matumaini na fursa," Rais wa Marekani Donald Trump alisema Ijumaa.
Akiongozwa na Makamu wa Rais JD Vance, Waziri wa mambo ya Nje Marco Rubio, na wajumbe kutoka DR Congo na Rwanda katika Ofisi ya Oval, Trump aliutaja mkataba huo wa amani "ushindi mtukufu".
"Haya ni mafanikio makubwa," Trump alisema, muda mfupi kabla ya kuongeza saini yake kwenye mkataba wa amani uliotiwa saini hapo awali na wajumbe husika wa Afrika.
Mkataba huo ulitiwa saini na mawaziri wa mambo ya nje wa Congo na Rwanda katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Rais Trump alijigamba kuwa anafanya mambo makubwa kuleta amani katika sehemu mbalimbali za dunia ambazo ziko kwenye vita, na pia alisema anakwenda kuzikutanisha Rwanda na DR Congo ili kutia saini makubaliano ya amani.
0 Comments