NA MATUKIO DAIMA APP.
DODOMA
Rais wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajia kutoa hotuba yake ya mwisho kwa Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama ishara ya kuvunjwa, tayari kwa uchaguzi Mkuu. Spika Tulia Ackson Jana katika Hotuba yake alibainisha kuwa Historia inaonesha zaidi ya asilimia 50 ya Wabunge wanapoingia katika uchaguzi hushindwa kurejea tena Bunge lijalo.
Kama ilivyo kwa mabunge yaliyotangulia, Bunge la 12 pia limeacha historia yake ya kipekee, likiwa na matukio ya kisiasa, kisheria na kijamii ambayo yataendelea kukumbukwa kwa muda mrefu.
Bunge hili litakumbukwa kwa kuwa na maspika wawili tofauti katika kipindi chake: Job Ndugai na Dkt. Tulia Ackson. Job Ndugai, aliyekuwa Spika wa sita wa Bunge, alijiuzulu Januari 6, 2022, baada ya kukosoa hadharani hatua ya serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kukopa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Kauli yake maarufu kwamba "kuna siku nchi itakuja kupigwa mnada" ilizua mjadala mkali wa kisiasa na ikahitimisha Uongozi wake.
Bunge la 12 pia liligubikwa na mvutano wa muda mrefu kuhusu uhalali wa ubunge wa Halima Mdee na wabunge wengine 18 wa viti maalum kutoka CHADEMA waliofukuzwa uanachama na kamati kuu ya chama hicho Novemba 2020. Licha ya kufukuzwa kwao, Bunge la 12 liliendelea kuwatambua kama wabunge halali, jambo lililozua sintofahamu ya kisheria na kisiasa.
Kwa kipindi kirefu, taarifa kuhusu matukio ya utekaji na watu kupotea zimekuwa zikiripotiwa kupitia vyombo vya habari na mitandaoni, huku Jeshi la Polisi likitajwa kuhusika. Mwaka 2025, Jesca Msambatavangu, mbunge wa Iringa Mjini kupitia CCM, alilihoji bungeni, lakini Spika Tulia Ackson alimwelekeza:
"Mheshimiwa Msambatavangu leta kama swali la msingi ili serikali iweze kujibu kikamilifu."
Alipoulizwa na vyombo vya habari Tanzania, kuhusu kutekwa kwa watu na Bunge kutojadili hoja hiyo, mbali na kusema neno kutekwa linatumiwa kwa mazoea bila ushahidi.
Bunge la 12 lilikuwa na upinzani mdogo zaidi kuwahi kushuhudiwa tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992. Mbunge wa CCM Luhaga Mpina aking'ara kwa kuwa na hoja kinzani zilizoitikisa serikali.
0 Comments