Na Pamela Mollel,Arusha
Wafanyabiashara wametakiwa kufanyia usafi maeneo yao ya biashara ili kuepuka kupigwa faini ya shilingi Elfu Hamsini,hali itakayosaidia wananchi kuzingatia usafi wa mazingira katika maeneo yao
Akizungumza katika uzinduzi wa Maadhimisho ya siku ya Mazingira Duniani,Katibu Tawala Wilaya ya Arusha Mh,Jacob Rombo ambaye alikuwa mgeni rasmi amewataka Wananchi pamoja na Wafanyabiashara kuhakikisha usafi wa mazingira ni kipaumbele cha kwanza
"Sisi tuna sheria ndogo inayotusaidia kusimamia usafi,ukitupa uchafu au eneo lako ni chafu utapigwa faini elfu hamsini,tunaona kabisa watu bado hawajaanza kupata machungu ya faini"anasema Rombo
Ameongeza kuwa watakuwa wakali katika kusimamia sheria hiyo kwa kuwa usafi ni jambo endelevu kwanzia kwenye makazi yetu na sehemu za biashara
Kwa upande wake Mkuu wa kitengo cha udhibiti wa Taka na usafi wa mazingira James Lobikoki ametaja maeneo ambayo zoezi hilo limefanyika kuwa ni eneo la soko kuu,stendi kubwa na mtaa wa Moivo jijini Arusha
"Kauli mbiu ya zoezi hili ni mazingira yetu,Tanzania ijayo,tuwajibike sasa lengo ni kudhibiti matumizi ya plastiki ambayo ndo taka hatarishi katika mazingira yetu"anasema Lobikoki
Maadhimisho ya siku ya mazingira Duniani yatafanyika jijini Dodoma tarehe 05/06/2025 ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mh.Rais MaMa Samia Suluhu Hassan
0 Comments