Header Ads Widget

MAPENDEKEZO KUHUSU HALI YA DEMOKRASIA NA MUAFAKA WA KITAIFA NCHINI KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA MWAKA 2025



1.0 Utangulizi

Watetezi wa Haki za Binadamu hapa nchini wana nafasi kubwa sana ya kuishauri jamii,

Serikali na vyama vya siasa kuhusu mambo mbalimbali yanayohusu ustawi wa jamii,

amani , haki za binadamu , demokrasia , utawala wa sheria na maendeleo ya nchi kwa

ujumla. Watetezi wa haki za binadamu wamekuwa ni wadau wakubwa hapa nchini katika

michakato yote ya uchaguzi. Mara kadhaa wameshiriki katika kudai maboresho , kutoa

elimu ya uraia, elimu ya mpiga kura na pia kushiriki kama waangalizi wa mwenendo wa

michakato ya kidemokrasia hapa nchini.

Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu ( THRDC) ni Mjumuiko wa Mashirika ya

Utetezi wa Haki za Binadamu zaidi ya 300 hapa nchini. Wanachama wa Mtandao wa

Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania mara kadhaa wamekuwa wakishauri viongozi wa

siasa hapa nchini pamoja na serikali kuhusu namna bora ya kutatua changamoto mbalimbali

za kijamii zikiwemo zinazoonekana kujitokeza wakati wote wa uchaguzi hapa nchini. Hivi

karibuni tumeshuhudia madai ya watanzania na vyama vya siasa kuhusu madai ya

umuhimu wa kufanya maboresho ya msingi kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Vyama vya upinzania pamoja na watanania wameendelea kutumia mbinu mbalimbali

kufikisha ujumbe wao kwa viongozi wa nchi kuhusu madai haya ya maboresho. Wengine

wamefanya mikutano ya hadhara na wengine wameendelea kutumia mitandao na vyombo

vya habari kuelezea madai haya. Asasi za Kirai hapa Nchini pia walitoa ilani ya Uchaguzi

ambayo imesisitiza na kushauri serikali pamoja taasisi zote zinazosimamia uchaguzi

kuhakikisha uchaguzi wa mwaka huu unakuwa huru na haki.

Tunatambua jitihada za Rais Samia kuhusu maboresho machachache yaliyofanyika katika

sheria zinazosimamia uchaguzi hapa nchini. Maboresho haya ni pamoja na wagombea wa

udiwani na ubunge kutopita bila kupingwa, Tume kuwa na mamlaka ya kuteua mtumishi

wa umma mwandamizi kuwa msimamizi wa uchaguzi na wafungwa kupiga kura kwenye

magereza. Maboresho mengine mazuri ni yale kuhusu upatikani wa wajumbe na viongozi

wa Tume ya Uchaguzi ambayo hata hivyo maboresho haya hayatumiki katika uchaguzi

huu. Pamoja na maboresho haya bado watanzania wanaona kuna maeneo mengine

yanayohitaji maboresho ya kikanuni , kisheria na kimatendo ili kuwa na uchaguzi huru na

haki. Umuhimu wa maboresho ya ziada ulidhihirika katika uchaguzi wa serikali za mitaaa

uliofanyika mwaka 2024. Uchaguzi huu ulikuwa na kasoro nyingi kama za wagombea wa

upinzani kuenguliwa ambazo pengine zingetoa nafasi ya kukaa kama Taifa kufanyia kazi

kasoro kama hizo na kuhakikisha hayatajirudia katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Tunasikitika kuwa pamoja na madai yote haya ya msingi kutoka kwa wananchi, AZAKI

na wanasisa hapa nchini hadi sasa hatujaona jitihada za haraka zinazochukuliwa na

mamlaka husika walau kufanyia kazi hoja hizi au kutafuta muafaka wa kitaifa katika

kufanyia kazi hoja hizi. Utamaduni wa kujadiliana na kukaa kwenye meza ya majadiliano

kutatua kwa pamoja changamoto za kitaifa unazidi kupungua na kufanya umoja na

mshikamano wa kitaifa kuwa mashakani. Falsafa za Mhe Rais za 4R kuhusu maridhiano

na maboresho haionekani ikitumika vyema katika nyakati hizi ambazo pengine ndio falsafa

hii ingepaswa kutumika zaidi.

Kama watetezi wa haki za binadamu tumeguswa na kuhuzunishwa na kitendo cha

kukamatwa na kufunguliwa kesi ya uhani kwa Mwenyekiti wa CHADEMA, Wakili Tundu

Lissu akiwa anafunga mkutano wa hadhara huko Wilayani Mbinga, Songea. Mazingira na

utaratibu uliotumika kumkamata Mhe Tundi Lissu haukuzingatia usalama wake, usalama

wa raia waliokuwa katika mkutano huo na pia usalama wa polisi wenyewe na amani ya

nchi. Nguvu iliyotumika ni kubwa wakati wa ukamataji na yenye kutia hofu kubwa kwa

wananchi kushiriki michakato ya uchaguzi. Jeshi la polisi kama walijua kuna tuhuma dhidi

yake wangemwita kwa wito au kumchukua kwa utaratibu wa kisheria nje na eneo la

mkutano halali kwa kuwa hata makosa anayostakiwa naye yanaonekana hayakutokea aneo

halilokamatiwa. . Hata hivyo, maneno anayotuhumiwa kuyatamka hayana uzito mkubwa

wa kufikia kuandikiwa kosa la uhaini. Uhaini ni kosa kubwa hapa nchini lisilokuwa na

dhamana na lenye adhabu ya kifo au maisha. Ni kosa ambalo kwa miaka kwa miaka mingi

sasa hapa nchini halijawahi kutumika pengine kutokan na uzito wake.

Ikikumbukwe kipindi hiki ni cha kuelekea uchaguzi na dhahiri kuwa lazima kutakuwa na

kauli mbalimbali kutoka kwa wanasiasa na wananchi ambazo zinaweza zisiwapendezeshe

makundi mengine au serikali. Kinachotakiwa wakati huu ni watu kuwa na uvumilivu wa

hali ya juu ili kuepuka kuvunja amani ya nchi. Pamoja na kuwa haki ya kujieleza ni muhimu

sana wakati wa uchaguzi , wananchi, watetezi na wanasiasa wote wanapaswa kuwa makini

na kauli zao ili kuepuka kujiingiza katika migongano ya kisheria. Wakati huo huo vyombo

vya dol ana viongozi walioko Madaraka wanapaswa pia kuwa makini na kuepuka kutumia

vyombo hivi vya dola vibaya dhidi ya makundi ya wanasiasa wa upinzani hapa nchini. Sisi

kama watetezi wa haki, amani na utulivu hapa nchini tunajukumu la kukumbusha haya na

kushauri makundi yote ya kijamii na serikali kuepuka kwa namna yoyote ile mazingira

ya kukandamiza demokrasia, kuvunja haki, kupoteza amani pamoja na kuvunja sheria za

nchi.

2.0 Mapendekezo Kuhusu Muafaka wa Kitaifa Kuelekea Uchaguzi Mkuu

Ili kulisaidia Taifa kwenda katika uchaguzi tukiwa wamoja na wenye utulivu Mtandao wa

Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) unapendekeza kupatikana kwa

“MUAFAKA WA KITAIFA” Muafaka huu wa Kitaifa ni muhimu sana kwa kuwa utatoa

nafasi ya hofu na duku duku zote kufanyiwa kazi kabla ya kwenda kwenye uchaguzi.

a) Wahusika wa Muafaka Huu

Suala la uchaguzi ni la Watanzania wote, hivyo tunapendekeza Muafaka huu wa Kitaifa

uwakusanye makundi yote ya kijaamii kama viongozi wa dini, asasi za kiraia, vyama vya

siasa na tasisi za kiserikali. Tunapendekeza mchakato huu wa kutafuta muafaka wa Kitaifa

usimamiwe na wazee wenye uzalendo na hekima hapa nchini na wasiokuwa na maslahi

yoyote na uchaguzi. Na tunashauri wadau wote washiriki mchakato huu wakiwa na roho

inayoamini katika dhana ya maridhiano na kuwa tayari kuachia kidogo ili kupata kidogo

(Win Win Situation). Kwa muda mrefu sana watanzania tumekuwa tukidhani swala la

maboresho na swala la uchaguzi ni swala la wanasiasa pekee. Sababu mojawapo pia

zilizochangia mambo mengi kukwama hapa nchini kama vile mchakato wa Katiba ni swala

la kuwachia na kuwahusisha wanasiasa pekee katika mambo ya msingi ya kitaifa. Madai

ya maboresho ya mfumo wa uchaguzi sio ya wanasiasa pekee na hayakuanza leo. Madai

haya yalianza toka mwaka 1992, lakini hadi leo maboresho yaliyofanyika ni machache

sana. Ili kufanikiwa katika Muafaka huu ni vyema makundi yote ya kijamii yakawa

sehemu ya mchakato huu kwa lengo la kufanyia kazi madai haya kabla ya kwenda kwa

uchaguzi.

b) Muda wa Muafaka

Mchakato wa Muafaka uanze mapema iwezekanavyo ili kutoa nafasi ya vyama vya siasa

na watanzania kuelekeza nguvu katika kujiadnaa na uchaguzi na sio kama ilivyo sasa

ambavyo muda mwingi unatumika kudai maboresho ya mfumo wa uchaguzi.

c) Hoja za Msingi wakati wa Mchakato wa Muafaka

Pamoja na kwamba washirika wa Muafaka watakuja na hoja zao zingine , tunapendekeza

msingi wa muafaka uwe ni kwenye mambo ambayo yamekuwa yakijotokeza katika

uchaguzi na kuathiri mchakato wa mzima wa uchaguzi. Tunafahamu kabisa kuwa msingi

wa changamoto za uchaguzi hapa nchini upo katika katiba na sheria zingine, lakini

kutokana na muda uliosalia katika kuelekea kwenye uchaguzi tunadhani yapo mambo

yanaweza fanyika kwa muda huu uliobaki endapo tutakwenda kwa njia hii ya muafaka wa

Kitaifa. Mambo mengine kama upatikanaji wa katiba mpya yanaweza kuwekwa kama

mambo yatakayofanyiwa kazi baada ya uchaguzi.

Maboresho na mambo ambayo yanaweza fanyiwa kazi yanaweza kuwa mengine ni ya

kisheria, kikanuni na mengine mengi ni ya kimtazamo na kiutendaji. Tunatambua kabisa

kuwa changamoto nyingi pia za kiuchaguzi zinachangiwa na aina ya wasimamizi, matendo

na mitizamo ya viongozi wakati wa uchaguzi. Changamoto hizi haziitaji mabadiliko yoyote

ya kanuni wala sheria bali msukumo wa pamoja kama Taifa kuondokakana na mambo

haya. Mfano matendo kama ya wasimamizi kukimbia wakati kurisha formu, kusumbua

mawakala wa vyama vya siasa, kuengua wagombea , matumizi ya vyombo vya dola

kusumbua vyama vya upinzani ni mambo ambayo yanaweza kudhibitwa kupitia Muafawa

wa Kitaifa Kuelekea Uchaguzi.

Tunapenda kuainisha masuala 10 ambayo yanahitaji kufanyiwa marekebisho au kuwekwa

saw ana kudhibitwa kwa pamoja ili kuhakikisha kwamba uchaguzi mkuu wa mwaka 2025

unakuwa wa huru na wa haki.

i) Wasimamizi wa uchaguzi wasiwe watumishi wa Serikali Pekee

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi inapaswa kuajiri watumishi wake na sio kutegemea

watumishi wa serikali pekee. Viongozi na Watumishi wa serikali ambao wanateuliwa

kusimamia uchaguzi sio watu huru, wenye maslahi na pia ni wengine wateule wa Rais

ambaye naye ni mgombea kwenye uchaguzi husika. Hoja hii ni ya muhimu sana na

uwezekano wa kufanyia kazi kabla uchaguzi ni mkubwa kama tutakuwa na Muafaka

wa Kitaifa.

ii) Tabia za maafisa wa uchaguzi kufunga ofisi hasa wagombea wa uchaguzi

wanaporusisha fomu wakati wa uchaguzi.

Kwa muda mrefu wasimamizi wa uchaguzi katika vituo wamekuwa na tabia ya kufunga

ofisi hasa wanaposikia kuwa wagombea wa upinzani wanataka kurudisha fomu za

uteuzi wa kuwa wagombea. Suala hili halihitaji mabadilikoya sheria bali ni kuwa na

Muafaka wa Kitaifa ambao suala hili litakuwa ni moja ya marufuku kuelekea uchaguzi

ujao.

iii) Wagombea kutoka vyama vya upinzani kuenguliwa.

Katika uchaguzi wa mwaka 2019, 2020 na 2024 wagombea kutoka vyama vya

upinzani wamekuwa wakienguliwa kwasababu mbalimbali ambazo hazina msingi

wala mashiko kama vile kutojua kusoma na kuandika, kukosea majina yao na

vyama vyao. Sisi tunaamini kwamba makosa katika kujaza fomu za uteuzi wa

wagombea hayapaswi kuwa ni hukumu ya kuwaengua wagombea ila wagombea

wanapaswa kupewa nafasi ya kurekebisha makosa hayo. Suala hili pia halihitaji

mabadiliko ya sheria kwa bali iwe ni mojawapo ya marufuku yatakayotokana na

Muafaka wa Kitaifa.

iv) Suala la mawakal kutoapishwa au kuondolewa kwenye vituo vya kupigia kura

Katika chaguzi zilizopita mawakala kutoka vyama vya upinzani wamekuwa

wakiondolewa kwenye vituo vya kupigia kura kwa nguvu. Takwa la mawakala

kuapishwa wakati wanasimamia uchaguzi ambalo ni zoezi la wazi halipaswi kuwa

kigezo kwani mawakala wengi wa upinzani wamezuiliwa kuingia vituo vya kupigia

kura kwa madai ya kwamba hawajaapishwa. Hii imepelekea mawakala wa vyama

vya upinzan kunyimwa barua za utambulisho au kukataa kuwaapisha au

kuwaapisha wakati tayari zoezi la uchaguzi linaendelea. Swala hili linaweza

jadiliwa kwa pamoja kama Taifa na kulipatia ufumbuzi kabla ya kwenda kwenye

uchaguzi.

v) Makosa ya kiuchaguzi kutambulika kama makosa ya jinai.

Wakati wa uchaguzi kumeibuka tabia ya kutumia makosa ya jinai kutia hofu

wanasiasa na wapiga kura. Vitendo vya kugeuza makosa ya uchaguzi na kuyafanya

kuwa makosa ya jinai yanaweza pia zungumzika bila kwenda kwenye maboresho

ya sheria. Uchaguzi haupaswi kuwa na makosa ya jinai.

vi) Vyombo vya habari na waangalizi uchaguzi kuzuiliwa kutoa taarifa

zinazohusiana na mapungufu ya uchaguzi siku au wakati wa uchaguzi.

Katika chaguzi zetu pamekuwa na udhibiti wa vyombo vya habari kurusha taarifa

ambazo zinaonyesha mapungufu katika zoezi la uchaguzi. Pia asasi za kiraia za

ndani zinazopewa kibali cha kutazama uchaguzi zimezuiwa kabisa kutoa maoni yao

wakati wote wa uchaguzi na badaye kutakiwa kuwasilisha taairifa ya uangalizi kwa

Tume ya uchaguzi ili kupata ruhusa ya kuitoa kwa umma.

vii) Matumizi ya nguvu kutoka kwa vyombo vya dola wakati wa uchaguzi.

Kumekuwepo na tuhuma ya vyombo vya dola hasa vyombo vya usalama kutumika

vibaya dhidi ya wapinzani wakati wa uchaguzi. Mara kadhaa wakati wa uchaguzi

wanasaia wa upinzani wamekuwa wakikamatwa , mikutano yao ikiingiliwa na wengine

kubambikiwa kesi mbalimbali na wakati mwingine wengine kupoteza maisha. Suala

hili linafanya mchakato wa uchaguzi usiwe na utulivu na kutia hofu kwa watanzania na

kuchangia kujitokeza kwa idadi ndogo ya wapiga kura.

Kwa mfano katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 katika jimbo la Hai, askari Polisi

alimwambia wazi mgombea wa upinzani kwamba hatashinda uchaguzi huo wa jimbo

la Hai. Askari huyo hakuwahi kuchukuliwa hatua zozote hadi hivi leo. Mfano hai

mwingine ni kukamatwa kwa Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Mhe. Tundu Lissu

wakati akihutubia mkutano wa hadhara Aprili 09, 2025 huko Mbinga na kusafirishwa

hadi Dar es Salaam na kufunguliwa kesi ya Uhaini. Vilevile mikutano ya hadhara

Songea iliyokuwa inaendelea ya CHADEMA kuzuiliwa na Jeshi la Polisi pasipo sababu

za msingi na za kisheria.

viii) Mapungufu mengi ya Sheria na Kanuni za uchaguzi.

Kwa mfano sheria hazitoi ulazima wa wakala au mgombea kuwepo eneo la

kuhesabia kura na kutokuwepo kwake hakuwezi kubatilisha chochote

kinachohusiana na matokeo ya uchaguzi. Mapungufu haya ya Sheria na Kanuni

yametumika vibaya hasa dhidi ya wapinzani ambapo mawakala wamekuwa

wakiondolewa kwa nguvu katika vituo vya kupigia au kuhesabia kura. Katika vituo

vya kupigia kura vilivyopo kwenye magereza, mawakala wa vyama na waangalizi

au watazamaji wa uchaguzi hawaruhusiwi kuingia kwenye vituo hivyo vya kupigia

kura. Katika vituo hivi mawakala, waangalizi na watazamaji wa uchaguzi

wanapaswa kuruhusiwa kuingia katika vituo hivyo. Muafaka wa kitaifa unaweza

jadili swala hili na kuanisha mambo ambayo yanaweza fanyiwa kazi kwa sasa na

yale ambayo yatafaniwa kazi baaada ya uchaguzi kama vile kupatikana kwa Katiba

mpya.

ix) Uwazi katika Mchakato wa Kuandikisha Wapiga Kura na Manunuzi ya Vifaa

vya Uchaguzi

Pia eneo hili limekuwa likilalamikiwa katika chaguzi zote na tunadhani inaweza

kuwa sehmu ya muafaka kuelekea uchaguzi mkuu ujao. Watanznia waachwe wawe

huru katika kuhoji na kudai taairfa za msingi kuhusu uchaguzi.

x) Suala usalama wa Kura na Utoaji wa Matokeo

Mara kwa mara kumekuwepo na malalamiko wakati wa uchaguzi kuhusu uwepo

wa kura feki , usalama wa kura na pia mchakato wa usambazaji wa matokeo kutoka

vituo kwenda maeneo ya majumuisho kutiliwa shaka. Mambo yote haya yanaweza

kufanyiwa kazi kwa pamoja kama sote tutakuwa na nia ya kuwa na uchaguzi huru

na haki.

3. Hitimisho

a) Tunashauri sana wadau wote wa uchaguzi , viongozi wa kisiasa, wananchi,

viongozi wa dini, wagombea na wasimamizi wa uchaguzi kuona umuhimu wa

kutafuta muafaka wa kitaifa kwa lengo la kuandaaa mazingira tulivu, huru na yenye

haki kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

b) Ni ukweli usiopingika kuwa hoja zilizotajwa hapo juu ndio zimekuwa kilio wakati

wote wa uchaguzi na sio busara kuelekea katika uchaguzi ujao bila kukaa chini

kama Taifa na kuzifanyia kazi.

c) Tunalishauri Taifa na viongozi wote wa nchi, vyama vya siasa, viongozi wa dini na

wananchi kuona umuhimu wa kuweka tofauti zetu pembeni na kuwa na Muafaka

wa Kitaifa kabla ya kuelekea kwenye uchaguzi ujao.

d) Ili kuweza kufikia hatua ya kuwa na Muafaka wa Kitaifa , tunashauri pia mashtaka

yanayomkabili Mkwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu yaondolewe kwa

mujibu wa sheria chini ya ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ili kupisha utekelezaji

wa mchakato huu wa Muafaka wa Kitaifa tunaoupendekeza. Mashtaka haya ni

makubwa na yanakwenda kuweka dosari kubwa katika uchaguzi wa mwaka huu

endapo ataendelea kushikiliwa kwa mashtaka haya ya uhaini. Sisi tunadhani bado

kuna nafasi ya kufanya marekebisho ya hati mashtaka haya yanayomhusu Tundu

Lisu na kuondoka kosa hili uhaini katika hati yake ya mashtaka ilia pate dhamana

na kurejea katika shughuli zake za kisasa na pia kushiriki mchakato huu wa

Muafaka wa Kitaifa tunaopendekeza.

e) Tunashauri wanasiasa wote nchini wakati huu wa kuelekea uchaguzi wajitahidi

sana kuchuja aina za matamshi wanayotoa wakati mwingine bila kujua madhara

yake au kwa nia nzuri lakini hupelekea kujiweka katika mazigira ya hatarishi zaidi.

f) Vyombo vya dola viepuke kwa namna yoyote ile kutumia mamlaka yao vibaya kwa

kuingilia uhuru wa vyama vya siasa kufanya siasa hapa nchini.

g) Kwa kuwa huu ni mwaka wa uchaguzi ni vyema kutambua kuwa haki ya kujieleza

inapaswa kulindwa kwa kila namna kwa kuwa ndio nyenzo muhimu wakati huu wa

uchaguzi. Serikali , taasisi za umma , wananchi na wanasisa mnapaswa kuwa na

uvimulivu na ustahimilivu wa maneno mengi ya kisiasa yanayotolewa wakati huu

wa uchaguzi.

h) Bado tunaamini kabisa maboresho ya msingi yanaweza kufanyika kwa kipindi

kilichobaki lakini inahitaji utashi wa kila kundi kuhakikisha hili linawezekana.

Maboresho mengine makubwa kama upatikanaji wa Katiba Mpya yanaweza kuwa

sehemu ya makubaliano ya muafaka kuwa yafanyike mara baada ya kumaliza

uchaguzi. Lakini kila kitu kiwe kimewekwa sawa katika Muafaka tunaopendekeza.

i) Tujenge utamaduni ya kukubali majadiliano na maridhiano wakati wote kama

Taifa, makundi yote yanayovutana katika jamii kuelekea uchaguzi hayana budi

kutumia busara na hekima na kukubali kujishusha na kutoa nafasi ya kuwa na meza

ya majadiliano. Tusiende kwenye majadiliano tukiwa na majawabu ya asilimia mia

moja bali tuwe tayari kupoteza na kupata na kuweka mbele uzalendo na utaifa.

j) Tunawasihi sana Wazee na Viongozi wastaafu wa Taifa wavunje ukimwa na

watumie busara na uzoefu wao kulishauri Taifa kukubali kuenenda katika

mazingiria ambayo kila Mtanzania ataona kuwa anatendewa haki katika Taifa lake.

k) Tuache kudhani na kuchukulia suala la uchaguzi kama ni jambo la wanasiasa pekee,

suala la uchaguzi linamgusa kila Mtanzania aliye hai leo na atakayezaliwa kesho.

Sote tunapaswa kuguswa pale tunapoona kuna mazingira yanapelekea kuvunja haki

za kiuchaguzi , kuvunja amani na utulivu hapa nchini. Kila mtu atumie nafasi yake

kuhakikisha tunatanguliza maslahi ya Taifa zaidi katika uchaguzi ikiwa ni pamoja

na kuhakikisha uchaguzi unakuwa wa haki,huru na wa amani.

l) Falsafa ya 4R ni wakati wake huu sasa kutumika ipasavyo ili kuhakikisha

tunakwenda katika uchaguzi tukiwa na umoja , uhuru , haki na

mshikamano.Tunamsihi sana na kumshauri Rais Samia kuona umuhimu na ulazima

wa kusaidia kufanyika kwa mchakato huu wa kupata muafaka wa Kitaifa Kuelekea

Uchaguzi kwa tunaamini hata yeye anaamini katika mazungumzo an majadiliano.

Onesmo Olengurumwa (Wakili)

Mratibu wa Kitaifa - Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania

Aprili 11, 2025 Dar es Salaam, Tanzania.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI