NA NAMNYAK KIVUYO, ARUSHA.
Kati ya vijana balehe 100, hamsini na nane wana changamoto ya udumavu pamoja na upungufu wa damu kutokana na kula vyakula visivyokuwa na virutubisho.
Hayo yameelezwa na afisa lishe mwandamizi kutoka wizara ya Afya Peter Kaja wakati akiongea na waandishi wa habari katika kongamano la vijana la taarifa sahihi juu ya virutubishi ambapo alisema kuwa wamewalenga vijana kwasabubu ni wahanga wakubwa katika jambo hilo.
"Kama serikali tumechukua hatua stahiki ambapo tumeweka miongozo, sera na sheria mbalimbali ili kuweza kukabiliana na changamoto hii lakini pia kuna vyakula vinne tunaenda kuongezea virutubishi mojawapo ni mafuta ya kula, unga wa Mahindi, unga wa Ngano pamoja na chumvi," Alisema Kaja.
Alieleza kuwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo wakapitie sheria ambayo mwanzo ilikuwa inawagusa wazalishaji wakubwa pekee na changamoto ikawa ni kwa wazalishaji wadogo ambao ndio sehemu kubwa wanailisha jamii na kwasasa wameshapitia sheria hiyo na kuwajumuisha.
"Inawataka kila mzalishaji kwenye hivi vyakula vinne chumvi, mafuta, unga wa ngano na unga wa mahindi kama anaenda kuuza kwenye jamii ataongeza vitamin za aina mbili ambayo ni folic acid, na B¹², pamoja na madini ya chuma na zinc,"Alieleza.
Alifafanua kuwa kwa upande wa chumvi kinachotakiwa kuongezwa ni madini Joto ili kuweza kupambana na changamoto za mimba kuharibika jambo amalo linaweza kusababishwa na ukosefu wa madini hayo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mwandamizi wa Kampuni ya Sanku inayoshughulika na teknolojia na urutubishaji, Gwao Omari Gwao alisema wanafanya kazi na wazalishaji 1200 katika mikoa 26 Tanzania Bara, lakini pia wananafanya kazi katika nchi ya Kenya na Ethiopia.
Alisema kampuni yao imebuni kifaa cha kuongeza virutubishi kinachoitwa Sanku na wanaongeza vurutubishi kwenye vinu vya mahindi vya kawaida ikiwa ni pamoja na kuwa kiwanda cha kutengeneza virutubishi nchini ambapo kwasasa virutubishi vya kuweka kwenye unga wa mahindi na Ngano vinapatikana nchini kwa bei rahisi.
" Tunafanya kazi na serikali kutekeleza mkakati wa urutubishaji na leo tumejumujka hapa kwaajili ya kuwatengeneza machampion ambao ni vijana kwaajili ya masuala ya lishe hususan eneo la urutubishaji na tunaamini kwa kuwapa elimu vijana hawa itasaidia kupeleka taarifa kwa jamii na katika maeneo yao ya masomo"Alisema Gwao.
" Vijana ni kundi maalum na muhimu katika masuala ya afya na uzazi, linahitaji makubwa ya madinina vitamin ndio maana tukaona ni sahihi kukutana na kundi hili na kuwapatia elimu ili wajue umuhimu wa lishe na namna ya kupata madini hayo na vitamin katika milo yao ya kila siku," Alifafanua
Aidha alieleza kuwa katika kundi la vijana walio mashuleni 52% wana tatizo la upungufu wa damu(Anemia) na kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano kwa takwimu za mwaka 2022 inaonyesha kuwa 58% wanachangamoto hiyo huku wanawake ikiwa ni asilimia 45.
Nao washiriki wa kongamano hilo Elizabeth Mathayo wa Taasisi isiyo ya kiserikali ya Elimu yetu, alisema wanashughulisha na kutoa elimu bure kwa watu wazima, watoto na wazee na wanatoa huduma ya lishe, lakini hawajuwi kipimo sahihi kinachotakiwa kuongezwa kwenye upande wa virutubisho.
"Kupitia kongamano hili wametusaidia kuelewa kipimo sahihi kinachotakiwa kuongezwa kwenye vyakula, ili kukuza afya ya watoto,watu wazima na wazee ila nitaenda elimisha wengine wanaojihusisha na masuala ya kuongeza virutubisho,"alisema
Naye mwanafunzi kutoka chuo cha Maendeleo ya jamii Tengeru Martin Mashaka alisema wanao wajibu wa kuielimisha jamii juu ya masuala ya urutubishwaji wa vyakula ili kuweza kulinda na kuboresha afya ya mama na mtoto.
Sambamba na hayo Afisa ustawi wa jamii kutoka wizara afya jamii Abubakary Haliye amewaasa waanawake wajauzito nchini kutumia vyakula vilivyoongezwa virutubishi ili kuepuka kupata changamoto za afya
Alisema uongezeaji wa madini ya vyakula kwenye vyakula unatoa uwezo kwa wanawake wajawazito kutopata changamoto kwa watoto wao tumboni kutokana na kula vyakula sahihi.
"Tumieni vyakula vyenye lishe bora ili kuepuka magonjwa mbalimbali sanjari na wanawake wajawazito kuhakikisha wanatumia dawa wanazopewa kliniki ili kujipeusha kuzaa watoto wenye changamoto za vichwa vikubwa, mdomo wazi," Alieleza
0 Comments