Na Moses Ng'wat, Mbozi.
MKUU wa Wilaya ya Mbozi, Ester Mahawe, ametoa siku 14 kwa mkaguzi wa ndani wa Halmashauri hiyo, kuhakikisha anafanya ukaguzi na kumpatia ripoti juu ya matumizi ya fedha za mfuko wa jimbo kuanzia mwaka 2021 hadi sasa katika majimbo yote mawili ya Mbozi na Vwawa, Wilayani humo baada ya Madiwani kulalamika.
Ametoa agizo hilo leo, Novemba 7, 2024, wakati akijibu malalamiko ya baadhi ya madiwani alipopewa nafasi ya kutoa salamu za serikali katika kikao cha baraza la madiwani kilichoketi kwa ajili ya kupitia taarifa za utekelezaji katika mwaka wa fedha 2024/25.
Mahawe amesema ripoti hiyo ya ukaguzi imfikie ndani ya siku 14 ikiwa na mchanganuo unaoonesha namna ya mchakato wa matumizi ya fedha hizo ambazo zilitolewa na serikali kwa ajili ya kusaidia shughuli za maendeleo.
"Fedha za mfuko wa jimbo si fedha za mtu, hivyo natoa maelekezo kwa Mkaguzi wa ndani kuhakikisha unafanya ukaguzi na ndani ya siku 14 uwe umenipatia ripoti na, pia Mkurugenzi pamoja na timu yako hakikisheni mnafanyia kazi suala hili". alisisitiza Mahawe.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya alitumia fursa huyo kuielekeza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Songwe nao kwenda kufanya uchunguzi wa kina kuhusu matumizi ya fedha hizo za mfuko wa majimbo hayo.
Awali madiwani wa kata za Nyimbili na Nambinzo, Tikson Nzunda, Gilbeth Vundwe, wakichangia taarifa ya fedha iliwasiliahwa na Makamu Mwenyekiti, Samsoni Nzunda, walihoji na kulalamikia mchakato wa matumizi ya fedha za mfuko wa jimbo katika majimbo yote mawili ya Wilaya ya Mbozi.
0 Comments