Header Ads Widget

HALI DUNI ZA MAISHA ZILIVYOCHANGIA AJIRA KWA WATOTO KATA YA KALENGA, IRINGA

 
Na, Herieth Molla, Iringa

Kata ya Kalenga, wilaya ya Iringa, ni mojawapo ya maeneo yanayoakisi hali ngumu ya maisha ya watoto wengi wa kike na kiume wanaojiingiza katika ajira za utotoni na hiyo imetokana naugumu wa Maisha ya walezi wao.

Watoto hao ambao wengi wao wanalelewa na bibi zao kutokana na wazazi wao kukimbilia miji mikubwa ili kupata Maisha bora, wamejikuta wakiingia kwenye harakati za kila siku za kutafuta chupa za maji za plastiki na vyuma chakavu ili waweze kuuza na kujipatia kipato kitakacho wasaidia wao na walezi wao.

 

Hata hivyo, hali hiyo hiyo inasababisha, watoto kushindwa kupata haki zao za msingi ikiwemo elimu wanayostahili, pamoja na kuwaweka katika mazingira hatarishi kiafya na kimwili.

 

Ajira za utotoni ni aina ya kazi ambazo mtoto haistahili kufanya kwa umri wake, Kazi hizi, kama vile kubeba matofali, kuuza chupa za plastiki na vyuma chakavu, humzuia mtoto kupata elimu na inaweza kuathiri afya, usalama, tabia, na makuzi yake.

 

Hata hivyo, watoto hao wamesema  wakiwa katika harakati za kutafuta vitu hivyo mekuwa  wanakutana na changamoto nyingi, ikiwa ni pamoja na unyanyasaji, ukatali na mazingira hatarishi.

 

Kwa upande wao, Wakazi wa Kata ya Kalenga wamesema kuwa sababu kuu, inayochangia watoto kujiingiza katika ajira za aina hiyo ni hali duni za familia.

 

Wamesema wazazi wengi wanashindwa kutoa huduma bora kwa watoto wao kutokana na hali duni ya kiuchumi, na wamnaume wengine wanakimbia majukumu yao ya familia na kuwaacha wake na watoto wao bila msaada wowote, huku baadhi ya watoto wakiachwa na bibi zao wakati wazazi wao wanapokimbilia miji mikubwa kutafuta maisha bora.

 

Martin Chuwa, Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Iringa na Mwenyekiti wa Maafisa Jamii Tanzania Bara, amesema kuwa wilaya ya Iringa inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya watoto waliotelekezwa na wazazi wao, na kwa sasa, wilaya hiyo ina jumla ya watoto 8,600 waliotelekezwa.

Chuwa amesema athari za ajira za utotoni si tu kwa maendeleo ya watoto, bali pia zinaongeza hatari ya watoto kukutana na unyanyasaji na ukatili wa kijinsia. Watoto wanajikuta wakiwa katika mazingira hatarishi, ambapo wanadhulumiwa na kukosa haki zao za msingi, kama vile elimu na usalama wa kisheria.

 

Mwanasheria wa kijitegemea, Baraka Kimata, amesisitiza umuhimu wa watoto katika jamii na kuzungumzia haki za watoto ambazo zimetambuliwa na sheria za kitaifa na mikataba ya kimataifa.

Kimata amesema kuwa watoto wanastahili kupata haki za msingi kama vile elimu, afya, usalama, na ulinzi wa kisheria, na kuongeza kuwa watoto wanapaswa kukua katika mazingira salama na yenye maendeleo, na ni kosa kwa mzazi au mlezi kumnyima mtoto wake haki hizo za kisheria.

 

Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) umeanzisha juhudi za kupambana na ukatili wa kijinsia, na sasa umejikita katika wilaya ya Iringa, hasa Kata ya Kalenga.

TGNP imefanikiwa kutoa mafunzo ya siku tano kwa wakazi wa kata hiyo, ambapo mafunzo haya yamelenga kuelimisha jamii kuhusu njia za kupambana na ukatili wa kijinsia na umuhimu wa kuwashirikisha wanaume katika masuala ya usawa wa kijinsia.

Rose Mwaisiko, Mwenyekiti wa Kituo cha Taarifa na Maarifa Kata ya Kalenga, amesema, kuwa mafunzo hayo yatasaidia kuongeza uelewa wa wazazi na walezi kuhusu athari za ajira kwa Watoto, Pamoja na  kupunguza changamoto.

 

Changamoto za ajira kwa watoto katika Kata ya Kalenga ni kielelezo cha hali ngumu inayokumba jamii nyingi nchini Tanzania, Watoto wengi wanajikuta wakifanya kazi ambazo siyo tu zinawazuia kupata elimu, bali pia zinawaweka katika hatari ya kutelekezwa na kukosa haki zao za msingi.

 

Hata hivyo, juhudi za mashirika kama TGNP na uhamasishaji wa jamii unaweza kusaidia kutatua changamoto hizi na kuhakikisha kuwa watoto wanapata fursa za kukua katika mazingira salama, bora, na yenye maendeleo.

Kwa pamoja, jamii, wazazi, na taasisi za serikali wanahitajika kuunga mkono juhudi hizi ili kuhakikisha watoto wanakuwa na maisha bora, mbali na kazi za kulazimishwa.

 

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI