NA MWANDISHI WETU, SUMBAWANGA.
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Mhe.Balozi Pindi Chana, ameweka jiwe la Msingi katika jengo la kituo kipya cha Afya cha Sumbawanga Asilia na kuwataka wananchi kukitunza vizuri kwa manufaa ya afya zao.
Tukio hilo limefanyika mapema leo Oktoba 2, 2024 katika muendelezo wa ziara ya Mhe. Chana katika Mkoa wa Rukwa.
Mhe. Chana amesema kituo hicho kimetumia takribani milioni 250 hivyo kitarahisisha upatikanaji wa huduma ya afya kitakapokamilika huku akimuelekeza Mkandarasi anayejenga Kituo hicho kukikamilisha kazi kwa wakati ili wananchi wapate huduma bora.
Naye, Kaimu Mganga Mkuu, Dkt. Louis Massawe amesema kwa sasa mradi uko katika hatua za mwisho za ukamilishaji ikiwemo uwekaji wa vigae pamoja na vioo.
Amesema mradi huo unajumuisha ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD), Maabara na Choo cha nje hadi kufikia sasa jumla ya shilingi milioni 163.8 zimeshatumika.
Kituo hicho cha Afya Sumbawanga Asilia kikikamilika kinatarajiwa kuhudumia wananchi zaidi ya elfu hamsini na Kata za jirani za Momoka na Mafulala.
Mwisho.
0 Comments