Header Ads Widget

SEKTA YA MADINI SINGIDA YAKUSANYA MADUHULI KWA ASILIMIA 164 ROBO YA KWANZA 2023/24



NA MATUKIO DAIMA APP 

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema kuwa Mkoa wa Singida umekusanya maduhuli ya Serikali kwa asilimia 164 katika kipindi cha mwezi Julai hadi Septemba 2023 ikiwa ni Robo ya Kwanza ya Mwaka wa Fedha 2023/2024.


Amesema hayo, leo Oktoba 17, 2023 wakati akizungumza kwenye Mkutano wa hadhara katika uwanja wa Shule ya Msingi Shelui wilayani Iramba mkoani Singida wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan mkoani humo.



“Mhe. Rais, Mkoa wa Singida ulipangiwa kukusanya shilingi bilioni 12 kwa mwaka huu wa fedha, lakini katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka zimekusanywa shilingi bilioni 4.9 sawa na asilimia 40 ya lengo la mwaka mzima wa fedha, ikiwa pia ni sawa na asilimia 164 ya lengo la robo ya mwaka, hongereni sana Mhe. Mkuu wa Mkoa Singida pamoja na timu yako kwa usimamizi wenu mzuri na kuongeza mchango wa Sekta ya Madini.” amesema Mavunde.


Akizungumzia maombi ya Mbunge wa Jimbo la Iramba Magharibi na Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba kuhusu kuwasadia wachimbaji wadogo wa Sekenke kupata leseni ya kuchimba katika eneo hilo linalofanyiwa utafiti, Waziri Mavunde amesema Wizara ya Madini ipo tayari kufuata maagizo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwasadia wachimbaji hao kwa kuzingatia taratibu za kisheria.


Ameongeza kuwa, maelekezo ya Rais Dkt. Samia ni kuhakikisha Taasisi ya Jiolojia na  Utafiti wa Tanzania (GST) inafanya utafiti wa kina wa Jiosayansi na kuwa na kanzidata ya kutosha kuhusu miamba yenye madini hapa Tanzania kwa lengo la kuwasaidia wachimbaji wadogo wasichimbe kwa kubahatisha.


Sambamba na hilo, Waziri Mavunde amesema kuwa Oktoba 21, 2023, jijini Dodoma Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya kukabidhi mitambo mitano ya uchorongaji kwa wachimbaji wadogo.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI