Na MatukioDaima App NJOMBE
Viongozi wa Kijiji cha Kipengele, Wilaya ya Wanging'ombe mkoani Njombe wamehukumiwa kwenda jela miaka 20 kwa kosa la uhujumu uchumi.
Watuhumiwa hao ni mwenyekiti wa Kijini, mtendaji, mhasibu pamoja na mwalimu mkuu wa shule ya msingi kijijini hapo.
Katika kesi hiyo no 01/2023 mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Njombe, Isack Mlowe watuhumiwa wanadaiwa kutumiwa fedha za kijiji kumlipa fidia mwanakijiji baada ya pikipiki yake ambayo ilihifadhiwa ofisi za kijiji hicho kuibwa.
Kesi hiyo ya Jamhuri dhidi ya Beatus Leonard Mdzovela, John Bosco, Otmary Mwinuka na Mdimbwi Japheti walishtakiwa kwa makosa ya kugushi muhtasari wa mahudhurio ya kikao cha wajumbe wa kijiji ili waweze kutoa fedha kwenye akaunti ya kijiji Shilingi milioni 2,670,000 kumlipa mwenye pikipiki na fedha nyingine waliitumia kwa mambo binafsi.
Jamhuri ilidai makosa hayo ni kinyume na kifungu 333,335(d)(1) na 337 vya Kanuni ya Adhabu sura ya 16 mapitio ya mwaka 2019, kutoa nyaraka za uongo kinyume na kifungu cha 342 cha sheria hiyo.
Mashitaka mengine ni ufujaji na ubadhirifu kinyume na kifungu cha 28(1) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Sura ya 329 Mapitio ya 2019, kusababisha hasara kinyume na aya ya 10 (1) ya nyongeza ya kwanza, pamoja na kifungu cha 57(1) na 60(2) vyote vya sheria ya Uhujumu Uchumi sura ya 200 mapitio ya mwaka 2019.
Upande wa Jamhuri uliwakilishwa na Mawakili Richard Malekano, Peter Majinge na Benjamini Sibanilo.
Baada ya Mahakama kusikiliza pande zote iliridhika kutendwa kwa makosa mawili kati ya manne ambayo walishitakiwa nayo.
Watuhumiwa hao walikutwa na hatia kwa makosa ya kutoa nyaraka za uongo, ufujaji na ubadhirifu na mahakama kuwatia hatiani washitakiwa watatu ambao ni namba 1,2 na 3 na kumwachia huru mshitakiwa namba 4 ambaye hakukutwa na hatia.
Aidha mbali na adhabu hiyo washitakiwa watatakiwa kulipa faini ya Sh 2,670,000 ambazo ni mali ya kijiji.
0 Comments