Header Ads Widget

UMOJA WA MITUME NA MANABII TANZANIA WATOA MSAADA KWA WAFUNGWA IRINGA.

 


Umoja wa mitume na manabii Tanzania tawi la Iringa wametoa msaada kwa wafungwa wa gereza la Iringa ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya wiki ya manabii na mitume yanayoendelea nchi nzima.


Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo Mwenyekiti wa umoja huo Bishop Doctor Samwel Shayo amesema wao kama umoja wa mitume na manabii wameguswa na kupelekea kutoa msaada wa majora matano(5) kwa ajili ya sare za wafungwa yenye thamani ya Shilingi Milioni Moja.


Pia amesema wamekusanyika toka siku ya Alhamisi katika ukumbi wa CCM Mkoa wa Iringa kwenye kongamano na mafundisho kwa ajili ya kuelimisha jamii na maombezi na dua katika kuelekea siku ya Jumapili ambapo kutakuwa na maombi maalum ya kuiombea nchi, kumuombea Rais na Serikali kwa ujumla, na mgeni Rasmi katika kuhitimisha kongamano hilo ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bi. Halima Dendego.


Nae Mkuu wa Gereza mkoa wa Iringa Mratibu Daniel Mwakapila ameshukuru kwa msaada huo huku akitoa rai kwa jamii kutoa misaada kwa wafungwa maana wanauhitaji na wengine wametengwa kabisa na jamii zao, ameongeza kuwa misaada hiyo inasaidia kuwafanya wafungwa warekebike maana wanajiona bado jamii ipo pamoja nao, hivyo basi inawafanya wabadilike.


Mchungaji Judith Reuben Sanga ambaye ni mjumbe wa umoja wa Mitume na manabii ametoa rai kwa wanawake kutoa misaada kwenye magereza maana waliopo magerezani sio kwamba wote wamekosea wengine walisingiziwa, wengine wameonewa kwa sababu mbalimbali, hivyo basi ameiomba jamii kuwakumbuka wafungwa maana kwa kufanya hivyo inawafanya waweze kubadilika na wasijione waliotengwa na kupelekea kurekebika kitabia.


Nae Mchungaji Getruda Eyamba ambaye ni Mweka Hazina wa umoja wa mitume na manabii amesema wajibu wao ni kuwapenda maana “Mungu mwenyewe ni upendo” na kuwaombea ili waweze kujua wanayoyafanya sio mazuri waweze kubadilika na kuishi kwa kumtegemea Mungu.


Doctor Amos Ponella yeye ni Katibu wa umoja wa Mitume na manabii amesema wajibu wao ni kuelimisha jamii katika maeneo mbalimbali ili jamii iweze kuepukana na ukatili wa kijinsia kwa sababu jambo hilo linaliathiri taifa na linaharibu nguvu kazi ya taifa kwa hiyo wao kama viongozi wa dini wanatoa elimu kwa kadiri wanavyoweza na ameitaka jamii kukataa na kupinga ukatili wa kijinsia kwa sababu pasipokufanya hivyo kinaandaliwa kizazi kibaya cha watanzania.




Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI