NA HADIJA OMARY LINDI
....TAASISI ya kuzuia na kupambana na Rushwa TAKUKURU Mkoa wa Lindi imefanikiwa kurejesha fedha kiasi cha shilingi 12,590,000/= zilizofujwa na baadhi ya watumishi wa Halmashauri tofauti katika mkoa wa Lindi
Hayo yameelezwa na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Lindi, Abnery Mganga alipokuwa anatoa taarifa za utekelezaji wa majukumu ya taasisi hiyo katika robo ya julai hadi septemba 2022
Mganga alisema fedha hizo zilitokana na ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo 13 yenye thamani ya shilingi bilioni 5.42 katika sekta za maji, Barabara, Afya na Elimu.
Alisema fedha hizo zilizofujwa na baadhi ya watumishi wa Halmashauri zilizotokana na utekelezaji wa miradi hiyo ziliweza kurejeshwa kwenye akaunti ya miradi husika kupitia udhibiti wa vitendo vya Rushwa katika utekelezwaji wa miradi ya maendeleo.
Hata hivyo Mganga alieleza kuwa katika utekelezaji wa shughuli za Taasisi hiyo kwa kipindi cha robo iliyopita msisitizo mkubwa ulikuwa ni katika kuzuia Rushwa ambapo watumishi wa mamlaka za Serikali za Mitaa na taasisi zingine zinapokea fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo katika Mkoa huo walipewa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa mbinu za ufuatiliaji fedha za miradi ya maendeleo ili kuwawezesha kujisimamia wenyewe.
Katika hatua nyingine Mganga alisema kuwa Licha ya kuhamasisha sana kuhusu Kuzuia Rushwa lakini kuna jumla ya Malalamiko 36 yalipokelewa na Taasisi hiyo ambapo kati ya hizo taarifa za Rushwa zilikuwa 17 na zisizo za Rushwa ni 19.
" taarifa hizi zilizopokelewa ni nusu ukilinganisha na taarifa zilizopokelewa katika robo kama hii mwaka 2021 hali ambayo inaashiria kuwepo kwa mafanikio katika mikakati ya kuzuia Rushwa "
0 Comments