Na Hamida Ramadhan Dodoma
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Selemani Jafo amesema kuwa makamu wa Rais Dkt Philip Mpango anatarajiwa kuzindua Sera mpya ya Taifa ya Mazingira ya mwaka 2021 katika maadhimisho ya wiki maalumu ya upandaji miti .
Hayo ameyasema leo wakati wa zoezi la Upandaji wa Miti katika eneo la Medeli katika wiki la upandaji miti ambapo amesema wameweka wiki maalumu ya upandaji miti kuanzia tarehe 7 na maadhimisho yatakuwa tarehe12 mwezi wa pili ambapo sera mpya ya mazingira ya mwaka 2021 itazinduliwa
"Leo nimefurahi sana katika kuona tunaendeleza zoezi la upandaji miti ndani ya Taifa letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na nimefarijika sana kuona wanafunzi kujitoa katika zoezi hili la kupanda miti," amesema Waziri Jafo
Na kuongeza kusema" Hapa tumekuja kuhakikisha tunafanya muendelezo wa zoezi letu la upandaji miti na na nimefurahi zaidi kuona hata ile kauli mbiu ya soma na mti wanafunzi wamejitokeza katika kupanda miti," amesema Jafo.
Aidha alitoa wito kwa wananchi kutumia vyema mvua zinazoendelea kunyesha kwa kupanda miti kwani matarajio ya serikali ni kupanda miti Milioni 276 kwa mwaka ambapo kwa kila Halmashauri itatakiwa kupanda miti Milioni 1.5 .
" Tusiache mvua hizo zipite bure tupande miti katika maeneo yetu na kwa wale wanafunzi ambao bado hawajapanda miti waliotakiwa kupanda waende wakapande ili kukamilisha ile kampeni ya soma na mti ," amesema Jafo.
Hata hivyo aliwashukuru wadau wote wa mazingira na kusema kuwa yale matamanio ya kuifanya Dodoma kuwa ya kijani inakwenda kutimia huku akiwataka familia nazo kupanda miti .
0 Comments