NA AMON MTEGA, SONGEA.
ASKOFU mkuu wa Kanisa la Evangelistic Assemblies Of God Tanzania (EAGT) Dr.Brown Mwakipesile amewataka wanadamu wamrudie Mungu kwa kuacha dhambi ili kuendelea kupata neema katika maisha yao yote ikiwemo na kukabiliana na mabadiliko ya tabia Nchi.
Wito huo ameutoa wakati akihubiri na kuzindua jengo jipya la kanisa la EAGT lililopo Mashujaa kata ya Mahenge Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma huku katika uzinduzi huo umehudhuliwa na watu mbalimbali ikiwemo viongozi toka Serikalini katika ngazi ya Wilaya na mkoa.
Akihubiri Askofu mkuu huyo kwenye ibada ya uzinduzi wa jengo hilo amesema kuwa wanadamu wengi siku hizi hawapati neema kwenye maisha yao ikiwemo na kuwepo kwa changamoto ya mabadiliko ya tabia Nchi ni kutokana na kutenda dhambi ambazo zimekuwa zikiwatenganisha kati yao na Mungu.
Askofu Mwakipesile amesema kuwa mpango wa Mungu kwa mwanadamu ni kutaka aishi kwa neema na siyo kumuangamiza hivyo ni vema wanadamu wakamrudia Mungu ili waendelee kupata neema katika maisha yao.
Katika hatua nyingine Askofu huyo amewapongeza waumini wa kanisa la EAGT la Mashuja-Mahenge kwa kufanikisha kujenga jengo kubwa la kuabudia jambo ambalo amesema ni kazi kubwa imefanyika huku akiwataka waumini hao walitumie kanisa hilo kikamilifu ili Mungu azidi kuwajalia.
Hata hivyo Askofu Mwakipesile ameongoza harambee ya kuchangia ununuzi wa vifaa vya mziki vya kanisa hilo kufuatia risala iliyosomwa na Gloria Lwomile kuwepo kwa changamoto ya uchakavu wa vifaa hivyo ambapo askofu huyo amechangia fedha zaidi ya shilingi laki tano(500,000.)huku wachungaji mbalimbali wa kanisa hilo nao pia waliunga mkono harambee hiyo.
Kwa upande mchungaji wa kanisa hilo Sozi Ngoso amesema kuwa muda mrefu waumini hao walikuwa na ndoto ya kujenga jengo kubwa la kuabudia jambo ambalo ndoto hiyo imetimia.
Naye diwani wa kata hiyo Mathew Ngalimanayo amezipongeza taasisi za dini kwa kazi nzuri ya kuwahubiria wanadamu neno la Mungu huku akiwataka vijana kujiepusha na vitendo viovu ili kujitengenezea maisha yao ya baadae.
MWISHO.
0 Comments