Katika kuelekea maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Haki za Mlaji Duniani, Tume ya Ushindani (FCC) imetangaza mkakati wa kuendelea kutoa elimu kwa umma ili kuhakikisha walaji wanapata bidhaa na huduma salama zinazokidhi viwango vinavyotakiwa.
Akizungumza tarehe 3 Machi 2026 jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, amesema tume hiyo itaendelea kuchukua hatua madhubuti kulinda maslahi ya walaji pamoja na kuimarisha ushindani wa haki sokoni.
Kwa mujibu wa Ngasongwa, Siku ya Mlaji huadhimishwa kila mwaka Machi 15, huku kilele chake kikiwa Machi 31. Mwaka huu maadhimisho hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo: “Bidhaa Salama, Imani kwa Mlaji.”
Kaulimbiu hiyo inalenga kusisitiza umuhimu wa kuhakikisha bidhaa na huduma zinazotolewa sokoni ni salama, zinakidhi viwango vya kitaifa na kimataifa, na hazihatarishi afya, usalama wala maslahi ya mlaji.
| Baadhi ya Watumishi wa FCC katika Mkutano na Waandishi wa Habari katika Mkutano wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC. |
Aidha, Ngasongwa ameeleza kuwa maadhimisho ya Siku ya Mlaji ni fursa ya kujenga imani ya walaji katika soko kwa kuhakikisha kunakuwepo uwazi, ubora na uwajibikaji miongoni mwa wafanyabiashara.
Amesema mlaji anayezingatia ubora huchangia ukuaji wa uchumi imara.
Aidha, wafanyabiashara wanaozalisha na kusambaza bidhaa bora hunufaika na mazingira ya ushindani wa haki, jambo linalochochea ubunifu, ufanisi na hatimaye kukuza uchumi.
Katika kuadhimisha siku hiyo, FCC imepanga kutoa elimu kwa wadau mbalimbali ili kuimarisha uelewa wa masuala ya ushindani na ulinzi wa mlaji. Lengo ni kuhakikisha wananchi wanafahamu haki zao na wanapata bidhaa pamoja na huduma zilizo bora na salama.
Kwa ujumla, maadhimisho ya mwaka huu yanatoa wito kwa wazalishaji, wasambazaji na watumiaji kushirikiana katika kujenga soko lenye ushindani wa haki na linaloweka mbele maslahi ya mlaji.
| Baadhi ya Waandishi wa Habari wakifatilia Mkutano wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC jijini Dar wa Dar es Salaam. |





0 Comments