Mkurugenzi wa Manispaa ya Kibaha, Dkt. Rogers Shemwelekwa, ameonesha kutoridhishwa na utekelezaji wa mradi wa uchongaji wa barabara katika mitaa ya Machinjioni na Kilimahewa, na kuagiza kazi hiyo irudiwe mara moja ili iwe katika kiwango kinachokidhi malengo ya serikali.
Dkt. Shemwelekwa ametoa agizo hilo tarehe 13/11/2025 katika ziara ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo katika Kata ya Tangini, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi inayoendelea katika maeneo Kata mbalimbali ya Manispaa ya Kibaha.
Amesema kuwa, barabara hizo ambazo zinagharimu shilingi milioni 30 kupitia mapato ya ndani ya Manispaa hiyo, hazijachongwa kwa ubora unaotakiwa na hivyo hazijakidhi lengo la serikali la kutatua kero za wananchi.
“Ndugu viongozi, nimekagua mradi huu wa barabara na niseme wazi sijaridhishwa na kazi iliyofanyika. Lengo la serikali ni kutatua kero za wananchi, lakini kwa hali hii sioni kama tatizo limepatiwa suluhisho. Naagiza mtendaji wa kata kuhakikisha barabara hizi zinachongwa upya, na nitarejea tena kukagua utekelezaji wake,” amesema Dkt. Shemwelekwa.
Aidha, Mkurugenzi huyo amewataka wananchi pamoja na viongozi wa ngazi ya kata na mitaa kuhakikisha fedha zinazotolewa kwa ajili ya miradi ya maendeleo zinatumika ipasavyo kwa malengo yaliyokusudiwa.
Katika hatua nyingine, Dkt. Shemwelekwa ameidhinisha ujenzi wa makaravati mawili eneo la shule ya msingi Mamlaka na kivuko Cha Kwa kwembe, katika maeneo yenye changamoto za mifereji ya maji, ili kupunguza kero zinazowakabili wananchi.
Manispaa ya Kibaha imetoa jumla ya shilingi milioni 420 kutoka chanzo Cha mapato ya ndani kwa ajili ya kutengeneza barabara za mitaa, ambapo kila kata imepatiwa shilingi milioni 30 ili kutatua changamoto za miundombinu kwa wananchi wake.








0 Comments