Header Ads Widget

TANZANIA YAJIPANGA KWA USHIRIKI WAKE MKUTANO WA COP30 NCHINI BRAZIL

 

Na Hamida Ramadhan, Matukio Daima Media Dodoma 

SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeanza maandalizi ya kushiriki katika mkutano wa 30 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi COP30 unaotarajiwa kufanyika kuanzia Novemba 10 hadi 21 mwaka 2025 katika jiji la Belém nchini Brazil

Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Cyprian Luhemeja amesema hayo jijini Dodoma wakati wa kufungua kikao cha kitaifa cha kupitia na kujadili vipaumbele vya nchi kabla ya kushiriki katika mkutano huo muhimu wa kimataifa


Amesema kuwa kabla ya mkutano huo mkubwa kutakuwa na vikao vya maandalizi kuanzia Novemba 4 hadi 9 mwaka 2025 ambavyo vitajumuisha mkutano wa wakuu wa nchi na serikali unaotarajiwa kufanyika Novemba 6 na 7 katika jiji hilo hilo la Belém

"Mkutano wa mwaka huu ni wa kihistoria kwa kuwa utafanyika katika Brazil ambayo ni miongoni mwa nchi zilizoanzisha mkataba wa mabadiliko ya tabianchi hivyo ajenda zitakazojadiliwa zinatarajiwa kuwa za kina na kuelekeza dunia katika kuchukua hatua madhubuti za haraka kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi baada ya miaka 33 ya  mkataba huo kuwepo, " Amesema Luhemeja


Aidha amesema Tanzania ilishiriki kikamilifu katika mkutano wa 29 wa COP29 uliofanyika mwaka 2024 jijini Baku nchini Azerbaijan ambapo ilipata mafanikio makubwa ikiwemo kupokea fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na mazingira ambayo baadhi yake tayari imeanza kutekelezwa kupitia taasisi mbalimbali nchini


Luhemeja amewataka wadau na washiriki wa kikao cha maandalizi kuhakikisha wanajadili kwa kina na kutoa mapendekezo yenye tija ambayo yataisaidia nchi kunufaika zaidi na mkutano wa COP30 hususan katika kupata fursa za kiuchumi kijamii na kimazingira zitakazochangia katika kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi nchini


Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI