Header Ads Widget

HEET YASAIDIA SUA KUANZISHA UTAFITI KUHUSU UAJIRIKA WA WAHITIMU WAKE WA MIAKA MITATU

 

Na Lilian Kasenene, Morogoro

Matukio DaimaApp 

CHUO Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (Higher Education for Economic Transformation(HEET), kimeanzisha utafiti maalum wa kufuatilia wahitimu wake wa miaka mitatu iliyopita (2021–2023), ili kubaini walipo, na shughuli wanazofanya.

Akizungumza katika semina ya kuwajengea uwezo watafiti kutoka SUA watakaokusanya taarifa hizo, Naibu Mratibu wa Mradi wa HEET-SUA, Dk Winfred Mbungu, alisema utafiti huo ni hatua muhimu katika kutathmini matokeo ya mitaala ya chuo na mchango wake katika kutoa elimu bora yenye tija kwa jamii.

Dk Mbungu alisema mbali na kubaini walipo watafiti hao pia wataangalia namna elimu waliyoipata imewawezeshaje kuajiriwa au kujiajiri.

“Tunataka kujua kama wahitimu wetu wameajiriwa, wamejiajiri, au wanaendelea na masomo. Taarifa hizi zitatusaidia kupanga mikakati madhubuti ya kuboresha ubora wa elimu na kuimarisha uhusiano kati ya mitaala yetu na mahitaji ya soko la ajira,” alisema Dk Mbungu.

Aliongeza kuwa ukusanyaji wa taarifa utafanyika kwa njia ya mtandao ili kupata takwimu sahihi na kurahisisha mipango ya maendeleo ya baadaye kulingana na hali halisi ya uajiri wa wahitimu.


Kwa upande wao, Dkt Noel Makwinya na Dk Shedrack Kitimu, wahadhiri wa SUA, walisema utafiti huo utasaidia kupima kiwango cha ufanisi wa ujuzi unaotolewa chuoni katika kuwaandaa wahitimu kujiajiri au kuajiriwa.

“Kupitia matokeo ya utafiti huu, tutaweza kubaini kama ujuzi wanaoupata wanafunzi chuoni unawawezesha kukabiliana na changamoto za maisha halisi ya kazi,” alisema Dk Noel.

"Taarifa hizi zitakuwa msingi wa maboresho ya mitaala ili iendane na mabadiliko ya kasi ya soko la ajira,"alisema Dk Kitimu.

Naye Mratibu wa Kipengele cha Uboreshaji na Ukuzaji wa Mitaala chini ya Mradi wa HEET-SUA,Prof. Jamal Athuman alisema kuwa katika mwaka wa masomo 2025/2026 chuo kitaanza kutekeleza mitaala mipya, hivyo ni muhimu kufahamu hali ya uajirika wa wahitimu waliopita kabla ya utekelezaji huo.

“Ni muhimu kujua hali ya uajirika wa wahitimu waliomaliza kabla ya kuanza kutumia mitaala mipya, ili tuweze kupima athari za mradi wa HEET katika kuboresha uajirika wa wahitimu wetu,” alisema Prof. Jamal.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI