Halmashauri Kuu ya Chama cha ACT Wazalendo kwenye kikao maalum kilichofanyika jana tarehe 5 Agosti 2025 kwenye ukumbi wa Hakainde Hichilema pamoja na mambo mengine ilipendekeza majina ya wagombea wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Urais wa Zanzibar.
Kwa mujibu wa Shangwe Ayo, Naibu Katibu wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma, ACT Wazalendo, kwa upande wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, majina yaliyopendekezwa ni;
1. Aaron Kalikawe
2. Luhaga Mpina
Kwa upande wa Urais wa Zanzibar Halmashauri Kuu imependekeza jina la Ndugu Othman Masoud Othman ambaye ndiye mwanachama pekee aliyechukua fomu ya kugombea nafasi hiyo.
Ndugu Othman Masoud Othman pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa Chama na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.
Majina ya wagombea yaliyopendekezwa yatawasilishwa kwa Mkutano Mkuu Taifa kwa ajili ya kupigiwa kura.
Katika hatua nyingine, Halmashauri Kuu ilipokea na kuridhia hatua ya mgombea wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ndugu Dorothy Jonas Semu kujitoa kugombea nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwenye maelezo yake mbele ya Halmashauri Kuu Ndugu Dorothy Semu ambaye pia ni Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo aliieleza Halmashauri Kuu kuwa alichukua hatua hiyo katika kutekeleza wajibu wake wa kiuongozi wa kukiwezesha Chama kutekeleza wajibu wake wa kimapambano wa kuiondosha CCM madarakani kwenye Uchaguzi Mkuu 2025 kwa kuzingatia mazingira ya kisiasa ya sasa nchini.
0 Comments