Na Fadhili Abdallah,Kigoma
MKUU wa mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro ameitaka wakala wa barabara nchini (TANROADS) kusimamia na kuziondoa changamoto zinazokabili mradi wa upanuzi na uboreshaji wa uwanja wa ndege wa Kigoma ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kuanza kufanya kazi.
Mkuu huyo wa mkoa ametoa maagizo hayo alipofanya ziara kutembelea na kukagua maendelea ya utekelezaji wa mradi huo na kusema kuwa kukamilika kwa mradi huo ni muhimu kwa maendeleo ya kiuchumi ya mkoa Kigoma na nchi kwa jumla.
Alisema kuwa TANROADS kama msimamizi wa mradi huo anapaswa kuhakikisha anawasiliana na mamlaka mbalimbali kuona namna zinavyoweza kusaidia na kuondokana na changamoto hizo na kwamba atatumia nafasi yake pia kuona analisimamia na kushughulia mradi huo ili kukamilika kwa wakati.
Sambamba na hilo Mkuu huyo wa mkoa Kigoma amewaonya wananchi wa mkoa huo kuacha wizi wa vifaa vya ujenzi wa mradi huo hasa sementi na nondo kwani wizi huo unaathiri kubwa kwa mradi huo na badala yake amewataka wananchi hao kuwa walinzi na kuuona mradi huo kama wao.
Awali Meneja wa Wakala wa barabara mkoa Kigoma,Narcis Choma alisema kuwa awali mradi huo ulioanza Septemba 2023 ulipaswa ukamilike August 25 mwaka huu lakini kwa sababu ya changamoto mbalimbali mradi huo umeongezewa muda hadi mwezi Desemba mwaka huu ambapo mradi ulipaswa kutumia kiasi cha shilingi Bilioni 46.6 lakini sasa utatumia kiasi cha shilingi Bilioni 51 hadi kukamilika.
MWISHO.
Mwisho.
0 Comments