Na Ashrack Miraji Matukio Daima
Katika juhudi za kukuza michezo na kuendeleza vipaji vya wanafunzi, Benki ya NMB imetoa msaada wa jezi za mpira wa miguu kwa vijana wanaoshiriki mashindano ya UMISSETA wilayani Same. Jezi hizo zimekabidhiwa rasmi kwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Same, Bi. Upendo Wella, na Meneja wa NMB tawi la Same, Bw. Saad Masawila.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo iliyofanyika Juni 2, 2025, Bw. Masawila alisema kuwa benki hiyo haijadhamiria tu kusaidia vifaa vya michezo, bali pia kuwasaidia wanafunzi waliofuzu ngazi ya taifa kwa kuwawekea fedha za kianzio kwenye akaunti maalum zitakazofunguliwa kwa majina yao.
“NMB tunaamini kuwa uwekezaji kwa vijana ni uwekezaji kwa taifa. Akaunti hizi zitawasaidia si tu kwa matumizi ya sasa bali pia kuwaandaa na tabia ya kujiwekea akiba mapema,” alisema.
Kwa upande wake, Katibu Tawala Bi. Upendo Wella aliipongeza NMB kwa mchango wao na kuwaagiza wachezaji kujituma na kuonesha nidhamu wakati wote wakiwa kambini ili waweze kuchaguliwa kuunda timu ya Mkoa wa Kilimanjaro itakayoshiriki mashindano ya UMISSETA kitaifa mkoani Iringa.
“Vijana hawa ni matumaini ya kesho. Wakifanya vizuri, si tu wanajenga majina yao, bali pia wanaitangaza Wilaya yetu ya Same. Nawasihi wajitume kwa moyo wote,” aliongeza Bi. Upendo katika hotuba yake ya kufunga rasmi kambi ya wilaya.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Same, Bw. Jimson Mhagama, alisisitiza umuhimu wa nidhamu kwa wachezaji, akisema kuwa tabia njema kambini ndiyo msingi wa mafanikio katika mashindano yoyote ya kimkoa au kitaifa.
Mashindano ya UMISSETA hutoa nafasi kwa wanafunzi wa shule za sekondari kuibua vipaji na kujifunza maadili ya michezo. Uungwaji mkono wa taasisi kama NMB unaendelea kuwa chachu muhimu katika maendeleo ya michezo ya shule nchini.
0 Comments