Katika siku za karibuni nchi yetu imeshuhudia kujirudia tena kwa matukio ya kikatili ambayo yamehusisha kuripotiwa kwa vitendo vya utekaji, utesaji na jana Jumapili Septemba 8, 2024 tukashuhudia tukio baya zaidi la mauaji ya kiongozi wa Chadema, Ali Mohamed Kibao.
Naungana na Watanzania wema wote kutoa mkono wa pole kwa familia, ndugu, jamaa, marafiki pamoja na viongozi na wanachama wa Chadema kwa msiba huo wenye kuhuzunisha sana.
Nimetiwa moyo sana na taarifa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ambapo alieleza kusikitishwa kwake na mauaji hayo na kutoa pole kwa wafiwa na wakati huohuo kuagiza uchunguzi wa haraka wa tukio hilo na mengine kama hayo.
Rais Samia hakuishia hapo, bali alitoa ujumbe mzito kwa kusema kuwa: "Nchi yetu ni ya kidemokrasia na kila raia ana haki ya kuishi. Serikali ninayoiongoza haivumilii vitendo vya kikatili vya namna hii."
(Imeandikwa na Rostam Aziz)
0 Comments