Mwenge wa uhuru baada ya kuwasili halmashauri ya wilaya Kasulu
Na Fadhili Abdallah, Kigoma
Halmashauri za wilaya nchini zimetakiwa kutumia fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya kuboresha miundo mbinu ya maeneo yao ya kutolea huduma ikiwemo ujenzi wa nyumba za watumishi ili kuvutia watumishi kudumu kufanya kazi na halmashauri hizo hasa maeneo yenye mazingira magumu.
Kiongozi wa mbio za mwenge kitaifa, Godfrey Mnzava alisema hayo wakati mwenge wa uhuru ukizindua nyumba nne za watumishi wa halmashauri ya wilaya Kasulu zinazotumiwa na familia 12 za watumishi wa idara ya afya ya halmashauri hiyo.
Mnzava alisema kuwa kutokuwepo kwa mazingira mazuri na wezeshi ya kufanya kazi ikiwemo nyumba na ofisi nzuri zinafanya watumishi kuomba uhamisho na kuhamia maeneo mengine hivyo ni jambo jema halmashauri ikatumia fedha zake za ndani kujenga nyumba za watumishi kama ilivyofanya halmashauri hiyo ya wilaya kasulu na kuipongeza kwa jambo hilo.
Akisoma taarifa kwa kiongozi wa mbio za mwenge kuhusu utekelezaji wa mradi huo mhandisi wa ujenzi wa halmashauri ya wilaya Kasulu, Julius Shirai alisema kuwa halmashauri imetumia kiasi cha shilingi Milioni 460 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.
Akizungumzia utekeleza wa mradi huo Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya wilaya Kasulu, Dk.Samistatus Mashimba alisema kwamba halmashauri imedhamiria kuwapatia watumishi makazi ya kuishi karibu na maeneo ya utoaji ili huduma hizo ziweze kupatika wakati wote na kwamba mpango wa ujenzi wa nyumba za watumishi ni endelevu kwa watumishi wote.
0 Comments