NA WILLIUM PAUL.
MBUNGE wa Jimbo la Moshi vijijini mkoani Kilimanjaro, Prof. Patrick Ndakidemi ametoa ushauri kwa Bodi ya mikopo nchini kuongeza nguvu katika ufwatiliaji wa mikopo ambayo wamekwishaitoa ili kuweza kurejeshwa kwa fedha hizo ziweze kuwasaidia Wanafunzi wengine.
Mbunge huyo alitoa kauli hiyo jana wakati akichangia bajeti ya Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia ambapo aliipongeza Wizara hiyo chini ya Waziri Prof. Adolf Mkenda ambapo alisema kuwa mwenendo wa Wiraza hiyo ni mzuri.
Alisema kuwa, yapo mageuzi makubwa ambayo yamefanywa na Wizara ya Elimu ambapo husimamia vizuri sekta ya Elimu kuanzia shule ya msingi, sekondari na Vyuo.
Alisema kuwa, kwenye kutoa mikopo Bodi hiyo irudi nyuma na kuangalia programa ambapo walikuwa wakitumia kuwapa mikopo kama Madaktari na watu wa sayansi wasije kuacha mtu kwani wao ndio wanaokuja kulisaidia Taifa.
“Wizara yetu ya Elimu imepata kiongozi bora na mchapa kazi msikivu , mnyenyekevu mwenye upendo na mshikamano wa hali ya juu na Wabunge wenzake” alisema Prof. Ndakidemi.
Alisema kuwa, lengo la mzazi yeyote anayempelekea mtoto wake chuoni ni kuhakikisha kuwa anapata elimu bora, ujuzi, uzoefu na mwishoni anakuwa na mafanikio kwa kuajiriwa au kuwa mjasiriamali hivyo ni vyema taasisi zote ambazo zimepewa dhamana ya kuwapa vijana elimu zikawa zimekamilika kikamilifu.
Mbunge huyo alisema kuwa, takwimu walizonazo zinaonyesha kwamba Taasisi nyingi hasa za Serikali na binafsi hapa nchini hazijakamilika ambapo zinaupungufu wa hali ya juu.
Alisema kuwa, kutokana na kutokukamilika kwa taasisi hizo kunaupungufu mkubwa wa Waadhiri kumepelekea ufundishaji, utafiti na kutoa huduma kwa jamii kumeathirika kwa kiwango kikubwa.
0 Comments