Wakili wa IPTL, Leonard Manyama akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa habari. (hawapo pichani).
NA MWANDISHI WETU, MATUKIODAIMA App
DAR
KAMPUNI ya kufua umeme wa dharula ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) inakusudia kwenda mahakamani kushtaki wamiliki, wahariri na wachapishaji wa Gazeti la MwanaHALISI endapo hawataomba radhi kwa madai ya upotoshaji wanaodaiwa kuufanya dhidi ya Kampuni hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari leo April 28, 2024 na Wakili wa IPTL, Leonard Manyama imesema hatua hiyo itafikiwa endapo menejimenti ya gazeti la MwanaHalisi itashindwa kuomba radhi, kukanusha habari hizo na kulipa fidia kama barua ya IPTL kupitia mawakili wake inavyowataka.
Kwa mujibu wa taarifa ya IPTL kupitia mwanasheria wake, Manyama unadai gazeti hilo kwa nyakati tofauti limekuwa likiandika habari za kuupotosha umma dhidi ya IPTL huku
ikitaja mojawapo ya habari zilizochapishwa na gazeti hilo Aprili 18 mwaka huu.
"Katika toleo hilo, gazeti hilo liliandika habari yenye kichwa kisemacho ‘Dili IPTL Laiva: Nyaraka zanyofolewa kumbeba Singasinga, Sasa kuchotewa zaidi Sh trilioni 1.8 ’ jambo ambalo IPTL inadai ni uongo." inasema sehemu ya taarifa hiyo ya IPTL na kuongeza kuwa
"Aprili 4, 2024 gazeti la MwanaHALISI liliandika habari yenye kichwa ‘IPTL rushwa tupu: Siri za kutaka kumlipa mabilioni mengine Singasinga zaiva,"imesema taarifa hiyo.
Taarifa ya Wakili Manyama imetoa ufafanuzi na kusema kwamba pamoja na mambo mengine kuwa IPTL ilianzishwa kwa ajili ya kuzalisha umeme wa Megawati 100 na kuliuzia Shirika la umeme, TANESCO.
Imesema kuwa ili kufanikisha lengo hilo IPTL ilisaini Mikataba mitatu kati yake na TANESCO pamoja na Serikali, Mikataba hiyo ilikuwa kwa ajili ya kununua umeme.
Kwa mujibu wa Mikataba hiyo, TANESCO ilitakiwa kununua umeme wote unaozalishwa na mitambo ya IPTL iliyopo Tegeta, Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam na kulipia malipo ya nguvu ya umeme.
Pia Serikali ilitakiwa kuhakikisha kuwa kama TANESCO inashindwa kulipa malipo hayo, basi Serikali inalipa na kuhakikisha kuwa leseni zote na vibali vyote vinavyohitajika ili IPTL izalishe umeme, vinapatikana bila kikwazo chochote.
Mwaka 1997 IPTL ilikopa fedha za Ujenzi wa Mitambao ya IPTL kutoka Benki Nne za Malaysia ambazo ni Bank Bumiputra Malaysia Berhad, Sime Bank Berhad, BBMB International Bank (L) Ltd na SIME International Bank (L) Ltd.
Mikataba hiyo ya Kununua Umeme ilikuwa ya muda wa miaka 20 kuanzia tarehe ambayo IPTL itaanza kuzalisha na kuuzia umeme TANESCO ambapo Mikataba hiyo ilianza Januari 15, 2002 na hivyo ilitakiwa kusitishwa Januari 15, 2022.
Mwisho
0 Comments