JESHI la Polisi mkoa wa Iringa linaendelea kumtafuta kijana Goodluck Mgovano mkazi wa mtaa wa Mlandege Kota katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa anayetuhumiwa kumuua kwa kumnyonga kwa kamba shingoni mtoto wake Alvin Mgovano mwenye umri wa miaka miwili na nusu kutokana na kurushiana maneno kati yake na mama wa mtoto .
Akizungumza kwa masikitiko makubwa mama mlezi wa mtoto huyo Magdalena Luvanda alisema kuwa baba mzazi wa mtoto Alvin alifika eneo ambalo mama mzazi wa mtoto anafanyia biashara na kumchukua mtoto huyo kwa lengo la kwenda naye nyumbani na ndipo alipofanikiwa kutenda tukio hilo la kikatili.
Baada ya kutenda tukio hilo la kumnyonga mtoto wake kwa kutumia kamba aliyoifunga katika mlango wa nyumba, baba mzazi wa mtoto huyo anayefanya kazi ya utingo wa magari ya mizigo, alijipiga picha mbili katika simu yake akiwa anamnyonga mtoto na picha nyingine alimpiga mtoto baada ya kumnyonga na picha nyingine alijipiga yeye pamoja na mtoto huyo (selfie) na kuandika ujumbe mfupi kwamba amemuua kwa sababu yeye ndiyo amemleta duniani na yeye ndiye anayemtoa pia ameagiza mtoto huyo azikwe pale atakapozikwa yeye.
Diwani wa kata ya Mlandege Wakili Jackson Chaula akizungumzia tukio hilo alisema kuwa tukio hilo ni la kwanza kutokea kwenye kata yake na kuwataka wananchi kuepuka na visasi kama hivyo na hata kama kuna ugomvi wa kifamilia ni vema kuumaliza kwa amani kuliko kufanya ukatili kama huo.
Kamanda wa polisi wa mkoa wa Iringa Allan Bukumbi aliwaeleza waandishi wa habari Leo ofisini kwake wakati akitoa taarifa za matukkio mbali mbali ya uhalifu ndani ya mkoa wa Iringa kuwa tukio la kijana huyo kumnyonga mtoto wake lilitokea majira ya jioni Ijumaa Octoba 20 mwaka huu.
"Inasemekana kijana huyo alichukizwa na maneno waliyorushiana na mzazi mwenzake hivyo kupelekea hasira zake kwa kuua mtoto wake na kuacha ujumbe wa maandishi kuwa mtoto huyo azikwe atakapozikwa yeye,hadi sasa bado tunaendelea kumtafuta kijana huyo " alisema kamanda Bukumbi .
Katika hatua nyingine kamanda Bukumbi alieleza mafanikio mbali mbali ambayo jeshi hilo imeyapata kutokana na kuwakamata watuhumiwa mbali mbali wakiwemo wa ubakaji ambapo baadhi ya kesi zimehukumiwa mahakamani ikiwemo kesi ya Suleman Wabuha (78) mkulima wa kijiji cha Idodi wilaya ya Iringa aliyehukumiwa kifungo cha maisha jela na kumlipa fidia muhanga kiasi cha shilingi milioni 5 kwa kosa l;a kubaka na kumuambukiza virusi vya UKIMWI muhanga .
Watuhumiwa wengine ni pamoija na Doto Kisinga (36) mkulima wa Ulata wilaya ya Iringa aliyehukumiwa kifungo cha maisha jela na kumlipa fidia muhanga ya shilingi milioni 5 kwa kosa la kubaka pia Richard Kinyamagoha (20) mkulima na mkazi wa Lukani wilaya ya Kilolo aliyehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela pamoja na kutakiwa kulipa fidia ya shilingi 300,000 kwa kosa la kubaka.
Aidha Kamanda Bukumbi alitaja watuhumiwa wengine waliopatikana na hatia na kufungwa kuwa ni Erick Kisoma (28) mkazi wa Mkalanga wilaya ya Kilolo aliyehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela pamoja na kutakiwa kulipa fidia ya shilingi 500,000 kwa kosa la kubaka pamoja na Dickson Mkana (30) mkulima na mkazi wa kijiji cha Igowole wilaya ya Mufindi aliyefungwa jela miaka mitatu na kutakiwa kulipa faini ya shilingi 300,000 kwa kosa la wizi wa pikipiki.
Katika hatua nyingine kamanda Bukumbi alisema jeshi la polisi mkoa wa Iringa katika oparesheni iliyofanyika kuanzia Oktoba mosi hadi Oktoba 30 lilifanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja aliyefahamika kwa jina la Adam Mgunda (29) mkazi wa Ilula kwa kosa la kupatikana na nyara za serikali ambazo ni meno ya Tembo vipande vitano ambavyo alikuwa amehifadhi kwenye mfuko wa sandarusi akiwa anasafirisha kwa kutumia usafiri wa pikipiki .
Tukio jingine ni la Oktoba 28 katika kijiji cha Kidamali wilaya ya Iringa kando kando ya barabara kuu ya kwenda Hifadhi ya Taifa ya Ruaha ambapo jeshi la polisi kwa kushirikiana na askari wa wanyamapori walifanikiwa kukamata vipande 25 vya meno ya Tembo ambavyo vilitelekezwa na mtu /watu wasiojulikana vipande hivyo vilikutwa kwenye mifuko mitatu ya Sulphate uchunguzi unaendelea ili kuwabaini wahusika .
Wakati huo huo jeshi la polisi limekamata silaha aina ya Gobore iliyotengenezwa kienyeji iliyotelekezwa katika shamba la David Mgava kijiji cha Kisovela kata ya Nduli Manispaa yab Iringa .
0 Comments