NA THABIT MADAI, ZANZIBAR
Jumuiya ya fasihi Zanzibar imeandaa tamasha kubwa la fasihi simulizi Zanzibar ambali linatarajiwa kuanza octobar 20 hadi 22 mwaka huu katika ukumbi wa Idrisa Abdul wakili huku Mgeni rasmi akitarajiwa kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Hussein Ali Mwinyi.
Akizungumza leo na Waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Jumuiya ya Walemavu Zanzibar UWZ Mhadhiri wa chuo Huria Tawi la Zanzibar Salma Omar Hamad amesema kwamba, lengo la Tamasha hilo ni kujenga hamasa ya kuandika vitabu kwa Waandishi chupikizi kuandika vitabu na kuitangaza Zanzibar.
"Tamasha hili litachochea Uandishi wa Vitabu vya Fasihi ambavyo vitatumika kutangaza Utalii wa Zanzibar," amesema.
Amesema, Tamasha hilo pua lina lengo la kujenga hamasa kwa Wananchi kupenda kusoma kazi za fasihi na kujifunza mambo mbalimbali.
"Tamasha hili litainua ari kwa Waandishi wa Vitabu pamoja na Wananchi kujifunza vitu mbalimbali kupitia wageni watakao hudhuria katika Tamasha hilo," ameeleza.
"Ukweli kwamba Asilimia kubwa ya Wananchi Visiwani hawana mazoea ya kusoma Vitabu kupitia Tamasha hili tutajenga ari ya kupenda kusoma vitabu na kujifunza mambo mbalimbali," ameongeza.
Hata hivyo ameeleza kuwa Tamasha hilo linatarajia kuhudhuriwa na Waandishi mbalimbali wa vitabu kutoka Ndani na Nnje ya Zanzibar.
"Hata hivyo Mwandishi mkongwe na Mshindi wa Tunzo ya Nobel anatarajiwa kuwepo katika Tamasha hilo," Amefafanua.
Nae Mwandishi Mkongwe wa Vitabu vya Fasihi na Mwandishi mwandamizi wa Habari Ali Saleh amesema kuwa katika Siku za Tamasha kutakuwa na uzinduzi wa vitabu cha Zubeda kachoka ambacho kimebeba Hadithi 13 ndani yake.
Amefahamisha kwamba, Katika Safari yake ya Uandishi wa Vitabu vya Fasihi ameandika vitabu vilivyobeba Maudhui mbalimbali kwa maslahi ya taifa.
Kwa upande wake, Mhandhiri Kutoka Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar SUZA Dkt. Mariam Jaffar Ismail amesema kwamba, katika tamasha hilo kutakuwa na shughuli mbalimbali kama vile Usiku wa Mashairi.
"Kutakuwa na Usiku wa Mashairi, Kazi za Watoto pamoja na siku malumu ambayo kutawasilishwa Umuhimu wa Matumizi ya Kiswahili, " ameeleza.
Tamasha hilo limeandaliwa na jumuiya ya fasihi Zanzibar kwa kushirikiana na wizara ya utalii na mambo ya kale ambapo kauli mbiu ikiwa ni Fasihi ya Zanzibar ulimwengu ndani ya Maneno.
0 Comments