Na Gabriel Kilamlya Matukio DaimaAPP NJOMBE
Serikali kupitia tume ya kudhibiti ukimwi Tanzania TACAIDS imeongeza bajeti ya mapambano dhidi ya ukimwi toka shilingi bilioni 14 katika mwaka wa fedha ulioisha hadi bilioni 25 katika mwaka huu mpya wa 2023/2024 ili watu wanaoishi na virusi vya ukimwi waweze kupata dawa kwa uhakika na kuendeleza shughuli zao.
Ripoti hiyo imetolewa na Naibu waziri ofisi Waziri mkuu sera bunge na Uratibu Mhe.Ummy Nderiananga alipowatembelea watu wanaoishi na virusi vya ukimwi katika halmashauri ya mji wa Njombe ambapo amesema lengo la serikali ni kuona WAVIU wanaendelea vyema na maisha yao huku wito ukitolewa kwa wanaume kujiunga kwenye vikundi pindi wanapobainika na VVU.
Mratibu wa ukimwi halmashauri ya mji wa Njombe Daniel Mwasongwe amesema halmashauri hiyo imefanikiwa kuwafikia wateja wapya 12717 katika huduma ya upimaji kwa kipindi cha mwezi januari hadi machi mwaka huu na kuwaunganisha na Huduma ya Dawa kwa waliokutwa na VVU.
John Msofu ni katibu wa Konga halmashauri ya mji wa Njombe na Rajab Safari ni katibu wa Kikundi cha watu wanaoishi na virusi vya ukimwi kata ya Ramadhani [JIUKU] kwa niaba ya WAVIU wanasema wamekuwa wakiendelea na shughuli mbalimbali za ujasiriamali ikiwemo kilimo cha Parachichi,Mbogamboga na Ufugaji jambo linalowasaidia kupunguza makali ya maisha.
Hata hivyo halmashauri ya mji wa Njombe inaomba kutengenezwa kwa mfumo wa Alama za vidole kwa watu wanaoishi na virusi vya ukimwi ili kurahisisha changamoto ya kupotea kwa watu wanaotumia dawa.
0 Comments