Na Gabriel Kilamlya Matukio DaimaAPP NJOMBE
Jumla ya watu 9 wameripotiwa kufikishwa Kwenye vyombo vya sheria mkoani Njombe kwa tuhuma za kuharibu vyanzo vya Maji ikiwemo kulima ndani ya mita 60 pamoja na kupanda miti isiyo rafiki na Maji hapo mwaka Jana.
Katika zoezi la upandaji miti katika vyanzo vya maji Kwenye vijiji vya Usalule,Sakalenga Ilembula wilayani Wanging'ombe na Howadi kibena mkoani Njombe wakati wa maadhimisho ya wiki ya Maji mwanasheria wa bodi ya Maji bonde la Mto rufiji Edward Izack amesema watu hao walikuwa wakikiuka sheria za mazingira.
Aidha Afisa maendeleo ya jamii bodi ya Maji bonde la mto rufiji Upendo Lugala anasema jumla ya miti 5000 aina ya mivengi iliyotolewa na mradi wa kuendeleza utalii kusini mwa Tanzania Regrow chini ya wizara ya maliasili na utalii imepandwa Kwenye vyanzo mbalimbali vya maji katika mkoa wa Njombe huku akiwataka wananchi kuitunza na kutoharibu vyanzo hivyo.
Wakishiriki zoezi la upandaji miti hiyo katika bonde la Maji la Mdzululu katika Kijiji Cha Usalule wilayani Wanging'ombe baadhi ya wananchi akiwemo Yuda Mtokoma mwenyekiti wa kijiji Hicho,Roy Kadege na Hosea Msemwa wamekiri kuwapo kwa baadhi ya waharibifu wa vyanzo vya maji lakini baada ya elimu kutolewa changamoto hiyo imepungua kwa kiasi kikubwa.
Sarah Mgaya ni Katibu wa jumuiya ya watumia maji bonde dogo la mto Mpando MWAM Usalule anasema Wameendelea kuimarisha vyanzo vya maji kwa kuvilinda na kupanda miti rafiki na maji Jambo linalosabisha kuwapo kwa ongezeko la maji kwa wananchi.
Mwezi machi kila mwaka Tanzania huadhimisha wiki ya maji kwa kufanya shughuli mbalimbali za uhifadhi wa mazingira na kufikia tamati machi 22.
0 Comments