NA HADIJA OMARY_LINDI……
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Lindi, imewafikisha mahakamani aliyekuwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Ruangwa Mkoani Lindi, Reuben Mfune(58) na aliyekuwa mtunza hazina wa halmashauri hiyo, Juma Masatu (56) kwa tuhuma za uhujumu Uchumi
Shauri hilo la uhujumu uchumi namba moja la mwaka 2023 linasikilizwa katika Mahakama ya Wilaya ya Wilaya ya Ruangwa, mbele ya hakimu Mkazi mfawidhi wa mahakama hiyo Mariam Mchomba.
Akiwasomea mashitaka mwendesha mashitaka wa Serikali, Peter Camilius mbele ya hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama hiyo alisema alisema wawili hao wameisababishia hasara halmashauri ya wilaya ya Ruangwa jumla ya shilingi 51,792,615. Iliyotokana na kuvunja mkataba na mzabuni ambae aliteuliwa kufanya kazi ya kuchimba visima kumi na moja vya maji katika baadhi ya vijiji vilivyopo katika halmashauri hiyo ya wilaya ya Ruangwa.
Camilius alisema tarehe 02.01.2014 halmashauri ya Ruangwa ilipokea shilingi Milioni 200 kutoka kwa katibu mkuu wa hazina. Ambapo fedha hizo zilipokelewa na kuwekwa kwenye akaunti ya maendeleo katika benki ya NMB namba 71101200032.
Alisema kiasi hicho cha fedha ambacho ilibidi kitumike kwa ajili ya kuchimba visima 11 vya maji katika vijiji vya Mbangala, Nandenje, Mtakuja, Likunja, Matambalale, Nandanga, Ng’alile, Nandanga, Mkaranga, Namilema, Namakuku na namahema hazikutumika kwa kusudio lililokuwa limekusudiwa. Badala yake takribani shilingi milioni 192 zilifanyiwa matumizi mengine.
Mwendesha Mashitaka huyo wa Serikali Alibainisha kuwa kitendo hicho kisababisha mkandarasi wa kampuni ya Maswi asilipwe shilingi milioni 182.7. Kitendo ambacho ni kinyume cha mkataba baina ya kampuni hiyo na halmashauri ya wilaya ya Ruangwa ulioingiwa tarehe 26.11.2014.
Mwendesha mashitaka huyo aliieleza mahakama hapo kuwa kitendo kilichofanywa na watumishi hao wa umma ni kosa kwa mujibu wa kifungu cha 10(1) jedwali la kwanza na kifungu cha 57(1) na 60(2) cha sheria ya uhujumu uchumi, sura ya 200 mapitio ya mwaka 2002.
Washtakiwa hao wote walikana shitaka lao ambapo mahakama imepanga kuanza kusikiliza shauri hilo tarehe 07.02.2023. na washitakiwa wote wapo nje kwa dhamana baada ya kukamilisha masharti ya dhamana.






0 Comments