NA CHAUSIKU SAID _MATUKIO DAIMAAPP MWANZA.
Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa Mh.Freeman Mbowe amemshukuru Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu kwa kuunga hoja za chama hicho na kuondoa zuio la mikutano hatua itakayosaidia kuchochea uchumi wa Taifa.
Mh.Mbowe ameyasema hayo leo Jumamosi Januari 21, 2023 wakati akizungumza kweye Mkutano wa kwanza wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Furahisha uliopo Wilaya ya Ilemela Jijini Mwanza.
Amesema amekaa kweye vikao mbalimbali na Rais kwaajili ya kutafuta maridhiano ya Taifa la Tanzania, namshukuru sana kwanamna ambavyo alikuwa mvumilivu wakati nikipeleka hoja za chama chetu.
" Mnyonge mnyongeni haki yake mpeni kwakweli Rais wetu ni msikivu sana anatambua umuhimu wa kuwa na Demokrasia katika nchi yetu hivyo tuendelee kumuombea kwa Mwenyezi Mungu azidi kumuongoza ili azidi kuliongoza Taifa katika misingi mizuri", amesema Mh.Mbowe
Amesema Kunabaadhi ya wanachama wa CHADEMA wanasema amekula asali ili awasaliti kitu ambacho kinamuumiza sana.
" Nilisimama miaka 30 iliyopita kuitafuta haki na ustawi wa nchi yangu hakuna idadi ya fedha wala wingi wa mali utakaonifanya nisaliti Chama changu nitaendelea kusimama kwenye haki siku zote", amesema Mh.Mbowe
Aidha, Mh.Mbowe ametumia nafasi hiyo kuwasihi watanzania kujenga Taifa lisilo na visasi badala yake wajibizane kwa hoja hatua itakayosaidia kuleta mabadiliko makubwa ya kiuchumi.
Kwaupande wake Katibu Mkuu CHADEMA Taifa John Mnyika, amesema ajenda yao kuu katika mikutano ya hadhara kwenye Mikoa mbalimbali ni kudai Katiba mpya na Tume huru ya uchaguzi.
Mnyika amesema kuondoa zuio la mikutano ni maamuzi mazuri ya kulijenga Taifa na tunaahidi mikutano yetu itakuwa ni fursa ya kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.
Nae Katibu Mkuu wa Baraza la wanawake (BAWACHA) Catherine Ruge, amesema miaka saba bila mikutano imekuwa ni chuo cha mafunzo kwao kwani sasa wako tayari kuwasemea wananchi kero zao.
Awali akizungumza kwenye Mkutano huo Mbunge mstaafu wa Mbeya Mjini Joseph Mbilinyi, amemshukuru Rais Samia Suluhu kwakuondoa zuio la mikutano ya hadhara iliyokuwa imedumu kwa muda wa miaka saba huku akisema watasimama imara kuhakikisha wanatetea maslahi ya wananchi ikiwa ni pamoja na kuzungumzia kero zinazoikumba jamii.
0 Comments