NA HADIJA OMARY,LINDI
WAZEE kutoka makabila mbali mbali ya Mkoa wa Lindi wanatarajia kufanya maombi maalumu kwa ajili ya kumkaribisha Rais wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anaetarajiwa kwenda Mkoani humo kwa ajili ya shughuli ya maadhimisho ya siku ya ukimwi Duniani Desemba mosi.
Hayo yamebainishwa leo na chama cha Wazee Mkoa wa Lindi katika kikao na waandishi wa habari wa Mkoa huo kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa chama cha mapinduzi CCM Mkoa wa Lindi.
Hii ni mara ya kwanza Rais samia kufika katika Mkoa huo wa Lindi toka alipoingia madarakani.
Akizungumza kwa niaba ya mwenyekiti wa chama cha wazee Mkoa, Mwalimu msaafu Zuhura Abdallah alisema kwa mila na utamaduni wa Mkoa huo wa Lindi wazazi wanakuwa wakifanya maombi maalumu kwa mtoto ambaye ajafika nyumbani kwa muda mrefu ama hajafika kabisa
" hivyo sisi wazee wa Lindi tumeamua kufanya maombi kwa chifu hangaya mama samia suluhu ili aendelee kutukumbuka wazee wa Lindi kama alivyokua anatukumbuka sana wakati akiwa makamu wa Rais" alisema Mwalimu Zuhura.
Mwalimu Zuhura aliongeza kuwa wameamua kufanya maombi hayo kwa sababu ya Mema mengi aliyoyafanya kwa wananchi wa mkoa wa Lindi toka alipoingia madarakani ambayo wao kama wazee wa Mkoa huo wanajivunia.
Aliyataja baadhi ya mambo ambayo Rais samia amewatendea wananchi wa Mkoa wa Lindi kuwa ni pamoja na ujenzi wa Hospitali ya Rufaa, uboreshwaji wa Madarasa , Zahanati na vituo vya Afya, Bandari ya uvuvi kilwa masoko pamoja na maandalizi ya mradi mkubwa wa kuchakata Gesi asilia Likong'o.
Hata hivyo wazee hao walimuhakikishia Rais Samia kuwa wako nae pamoja na kwamba wanamuheshimu kama kiongozi wao wa machifu hivyo wako tayari kushirikiana nae kwa maslahi ya Lindi na Tanzania kwa ujumla.
0 Comments