Header Ads Widget

TCRA YATOA ELIMU KWA WANAFUNZI CHUO CHA SAUT JUU YA MATUMIZI YA MITANDAO

 

Meneja wa TCRA Kanda ya Ziwa, Francis Mihayo akifafanua jambo kwa waandishi wa habari mara baada ya kuwasilisha mada kuhusu matumizi sahihi ya teknolojia na mitandao ya kijamii kwa wanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino (Saut) Mwanza.

                                XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Mamlaka ya Mwasiliano Tanzania (TCRA) Kanda ya Ziwa imewanoa wanafunzi wa elimu ya juu kuhusu matumizi sahihi ya maendeleo ya teknolojia ikiwemo mitandao ya kijamii ili kuwaepusha na makosa yanayoweza kuwaingiza kwenye migongano na mamlaka za usimamizi na utekelezaji wa sheria.

 

Akizungumza na wanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino (Saut) jijini Mwanza, Meneja wa TCRA Kanda ya Ziwa, Francis Mihayo amewashauri vijana nchini kutumia maendeleo ya teknolojia kama nyenzo ya kutanua wigo kujifunza na kujiendeleza  kiuchumi badala ya mambo yanayokiuka sheria ikiwemo kutuma ujumbe na picha zinazokiuka maadili na sheria.

“Sekta ya mawasiliano ni msingi mkuu wa ujenzi wa uchumi duniani kwa sasa; nawasihi wanafunzi wa elimu ya juu kuitumia kwa manufaa yao kielimu na kuichumi kupitia fani zao,” amesema Mihayo

 

Amesema kutokana na umuhimu wa maendeleo ya teknolojia, TCRA imekuwa ikitumia mikusanyiko ikiwemo taasisi za elimu ya juu kuelimisha umma, hasa vijana namna ya kutumia teknolojia kwa usahihi huku akiushukuru uongozi wa Saut kwa kutoa fursa kwa mamlaka hiyo kukutana na kuwaelimisha wanafunzi wa chuo hicho.

 

 “Baadhi ya wanafunzi wapya wanatoka maeneo na mazingira ambayo hawakuwa na matumizi makubwa ya mitandao au walikuwa wanaitumia kwa usimamizi na uangalizi wa wazazi na walezi wao; sasa wamefika chuoni ambako wanapaswa kujisimamia wenyewe, ndiyo maana tunawapa msingi wa matumizi sahihi ya mitandao,” amesema Mihayo


Askari Polisi kutoka kitengo cha makosa ya mitandao, Musa Zuberi amesema takwimu za makosa ya mitandaoni yanayoripotiwa polisi  inaonyesha kuwa wanafunzi, hasa wa elimu ya juu ni kati ya makundi ya kijamii yanayojikuta kwenye migogoro na mamlaka za dola kwa matumizi mabaya ya mitandao.

 

“Kesi za picha zisizofaa na udhalilishaji kupitia mitandao ya kijamii ni miongoni mwa makosa ya kimtandao yanayofanywa na baadhi ya wanafunzi wa elimu ya juu; nawasihi kila mmoja atumie vema mitandao hii kuepuka mkono wa dola,” amesema Zuberi

 

Fauzia Hashim, mmoja wa wanafunzi wa mwaka wa kwanza Saut ameishukuru TCRA kwa elimu ya matumizi sahihi ya teknolojia ambayo itawawezesha kuepuka makosa ya kimtandao.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI