Wakala wa barabara mijini na vijijini Tarura mkoa wa Njombe umetakiwa kuweka wazi mpango kabambe wa ujenzi wa barabara(Master Plan) utakaoonyesha namna miundombinu ya barabara itakavyokwenda kushughulikiwa.
Mkuu wa mkoa wa Njombe Antony Mtaka wakati akifungua kikao cha bodi ya barabara amesema anachotamani kukiona ni matokeo ya ujenzi wa barabara hususani za vijijini chini ya Tarura.
Mtaka amesema anataka kuona mpango kabambe wa ujenzi wa barabara(Master plan) utakaonyesha ni kwa kiasi gani miundombinu ya barabara za vijijini zinakwenda kutekelezwa na zilete manufaa kwa wananchi.
Katibu tawala mkoa wa Njombe Judica Omary amesema Mkoa wa Njombe una Km 1188 za barabara zinazohudumiwa na Tanroads na Km 5200 zinahudumiwa na Tarura.
Mjumbe wa halmashauri kuu ya CCM taifa mkoa wa Njombe MNEC Daniel Okoka kwa niaba ya mwenyekiti wa CCM mkoa wa Njombe Deo Sanga amesema fedha zote zinazoletwa zinapaswa kusimamiwa kikamilifu na zijenge barabara kwa kadri ya mahitaji ya sasa.
Meneja wa Tanroads mkoa wa Njombe Mhandisi Lucy Shalua amesema wanaendelea na ujenzi wa barabara mbalimbali ambapo jumla ya KM 107.4 zimekamilika na zipo kwenye matazamio.
Meneja wa Tarura mkoa wa Njombe Mhandisi Gerlad Matindi amesema Km 5208 wanazozisimamia hali yake kwa sasa sio nzuri hivyo jitihada kubwa zinahitajika kwa kuwa hawana Km nyingi za lami.
Amesema wamepokea kiasi Cha shilingi Bilioni 20.34 kwa ajili ya matengenezo ya barabara na kiasi Cha shilingi Bilioni 16 zimeshatumika.
0 Comments