Header Ads Widget

KANISA LA KRISTO LASAIDIA WAZEE WASIOJIWEZA MBARALI


Na Matukio daima media , Mbeya

WAUMINI wa kanisa la Kristo lililopo Kata ya Chimala wilayani Mbarali mkoani Mbeya wametoa msaada wa vitu mbali mbali kwa wazee 30 wasiojiweza ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya wazee Duniani.


Vitu vilivyotolewa kwa wazee hao ni kilo 60 za sukari ,sabuni , blangeti tano , mashuka matano , pamoja na nguo kwa wazee 30 wasiojiweza .


Akizungumza  na mtandao huu leo mara baada ya vifaa hivyo kukabidhiwa kwa wazee,Mwenyekiti wa umoja wa wazee Kata ya Chimala,Wily Chenelo kuwa kwa kata ya Chimala pekee  wana idadi kubwa ya wazee wasiojiweza ambao wana uhitajhi mkubwa hasa wanawake  na mbaya zaidi hawapati TASAF.



Mzee Chenelo alisema kuwa  licha uhitaji walionao wazee  hao  lakini bado wana familia  ambazo zinawategemea ambao kwa kiasi kikubwa ni wajukuu ambao wameachiwa na watoto wao na wao kushindwa kuwakumbuka wazee wao.


Hata hivyo Mwenyekiti huyo aliomba serikali iwaangalie wazee wanaojishughulisha na kilimo wapatiwe ruzuku ya  pembejeo ili waweze  kupata  kwa bei nafuu ilim kila mzee aweze kumudu gharama hizo.


Akizungumzia kuhusu vyeti vya msamaha  wa matibabu  kwa wazee  hawapati  hivyo kulazimika kupokea malalamiko ya wazee mara kwa mara kuhusu vyeti hivyo.


“Ndugu yangu mwanangu hali ni mbaya kwa wazee kwani hata huu msaada waliopatiwa kutoka  kwa waumini wa Kanisa la Kristo bado hautoshelezi mahitaji ya wazee kutokana na kuwa wengi wazee hao ,hivyo tunaomba watu mbali mbali wajitokeze kusaidia kundi hili la wazee ili wapate mahitaji muhimu hususani nguo , chakula na mahitaji mengine muhimu “alisema.


Kwa upande wake Msaidizi wa Mchungaji wa kanisa la Kristo lililopo kata ya Chimala wilaya ya mbarali ,Meshack Malongo  alisema kuwa waliguswa kuwasaidia wazee wasiojiweza kwani Mungu anawahitaji waweze kusaidiwa  kutokana na  hali halisi ya uzee waliyonayo.


Aidha Malongo alitoa wito  kwa makanisa mengine kuwa na ibada iliyo njema kwa kuwaombea wazee wasiojiweza ikiwa ni pamoja na kuwasaidia  wazee wasiojiweza.


“Sisi binadamu  kila mmoja ana moyo wake  hivyo sisi viozi wa dini tunapaswa  kuwaelekeza waumini wetu  kujua umuhimu wa kujitoa  kwa ajili ya kuwasaidia  wazee wetu wasiojiweza kwani wapo wazee wengine hawana uwezo kabisa”alisema kiongozi huyo wa dini .


Kwa upande wake Afisa Ufuatiliaji wa Asasi isiyokuwa ya kiserikali inayojishughulisha na masuala ya wazee (KIWWAUTA) Mussa Mchalo alisema kuwa asasi hiyo imekuwa bega kwa bega na wazee katika kuwasaidia kupitia kwenye mabaraza ya wazee .


Mwisho.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



BBC NEWS