Na Mapuli Misalaba, Shinyanga
Wanakikundi wa jukwaa la mtandao wa WHATSAPP linalojulikana kwa jina la “Together we Fight” la Mkoani Shinyanga wametoa msaada wa vitu mbalimbali ikiwemo vyakula, vifaa vya shule pamoja na nguo katika kituo cha kulelea Watoto wenye ulemavu wa akili na usonji (Brothers of charity) kilichopo kata ya kitangili Manispaa ya Shinyanga.
Akizungumza baada ya kukabidhi msaada huo mratibu wa jukwaa hilo GWAKISA MWASYEBA ameeleza kuwa msaada huo utasaidia kuwawezesha watoto hao na kwamba wametoa msaada huo ikiwa ni sehemu ya matendo ya huruma kwao.
Mwasyemba amesema wametoa vitu mbalimbali ikiwemo mchele kilo 200, unga kilo 100, maharage , Sabuni, nguo,daftari pamoja na kalamu ambavyo thamani yake ni zaidi ya shilingi Milioni moja.
Mratibu huyo wakati amesema kuwa kikundi hicho cha mtandao wa WHATSAPP kinachojulikana kwa jina la “Together we Fight” kimeendelea kusaidia vituo mbalimbali vyenye watoto wenye mahitaji maalum kupitia majitolea ya mtu mmoja mmoja lengo ni kupunguza ama kumaliza changamoto.
Amesema kikundi cha “Together we Fight” ambacho kwa sasa kinawanachama 150 kilianza kutoa mahitaji maalum Mwaka 2020 katika sehemu tofauti ikiwemo Hospital ya rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, ambapo kikundi hicho kilitoa msaada wa mitungi 10 ya hewa ya Oksijeni kwa ajili ya kusaidia wagonjwa wanaopata changamoto ya upumuaji.
Kikundi cha “Together we Fight” kilitoa pia msaada wa vitu mbalimbali ikiwemo vyakula, vifaa vya shule pamoja na nguo kwa wasichana wanaolelewa katika kituo cha Agape ambapo leo ilikuwa ni mwendelezo wa majitoleo hayo katika kituo cha kulelea Watoto wenye ulemavu wa akili na usonji (Brothers of charity) kilichopo kata ya kitangili Manispaa ya Shinyanga.
Mratibu Mwasyemba amesema lengo la wanakikundi hao kutoa msaada huo ni kutaka kujenga utamaduni wa kutumia mitandao ya kijamii kufanya shughuli za kijamii badala ya kutumia majukwaa hayo kwa matumizi mabaya.
Amewaomba wananchi kujenga utamaduni wa kusaidia watu wenye mahitaji maalum ili kupunguza changamoto zanazowakabili ambapo pia amewaomba kujiunga na kikundi hicho ambacho bado kinaendeleo kusaidia watu wenye uhitaji.
Amesema jukwaa hilo la mtandao wa WHATSAPP linalojulikana kwa jina la “Together we Fight” la Mkoani Shinyanga linawanachama wanaotoka mikoa mbalimbali ambapo ametumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi wote kujiunga na jukwaa hilo ili kusaidia watu wenye uhitaji ambaye pia ametaja namba ya Admin wa kikundi hicho kwa yeyote atakayehitaji kujiunga na jukwaa hilo 0766123458 ambayo ndiyo namba ya Admin mkuu wa kikundi.
Baadhi ya wanachama wa jukwaa hilo ambao wameshiriki zoezi la kukabidhi msaada wa vifaa hivyo ambapo pamoja na mambo mengine wamesema wanaguswa kutoa msaada huo kwa lengo la kujenga mahusiano masuri na watu wenye mahitaji ikiwa ni pamoja ja kuwafariji na kuonyesha upendo wa dhati kwao, huku wakitoa wito kwa wananchi kujenga tabia ya kutenda matendo ya huruma kwa watu wenye mahitaji maalum
Akizungumza baada ya kupokea msaada huo Mkuu wa kituo hicho Brother George Paulo amewashukuru wanakikundi kwa kutoa msaada huo ambapo amesema msaada uliotolewa utasaidia kupunguza changamoto zinazowakabili watoto hao.
Aidha Mwenyekiti wa mtaa wa Majengo mapya kata ya Kitangili Mohamed Juma ametoa wito kwa wazazi kupeleka watoto wenye changamoto zinazohitaji msaada huo kwenye vituo husiki ili waweze kupata msaada.
0 Comments