Elizabeth Ntambala
Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la AGRA na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Jakaya Mrisho Kikwete amewapongeza wanachama wa chama cha ushirika Mpui kwa mafanikio waliyoyapata kwa kuongeza tija katika uzalishaji wa zao la mahindi toka wastani wa gunia sita(6) kwa ekari hadi kufikia gunia 20.
Akizungumza na wananchi wa kijiji cha Mpui wilaya ya Sumbawanga leo Rais Mstaafu Kikwete alisema kazi ya shirika hilo la AGRA ni kusaidia wakulima wadogo kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao hususan ya chakula hatua inayowawezesha kuwa na usalama wa chakula katika kaya na taifa.
"AGRA shabaha yake ni kusaidia wakulima wadogo kuongeza tija na uzalishaji mazao ya chakula katika kaya na ziada itakayopatikana iwawezeshe kupata kipato" alisema Kikwete.
Awali Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti alimpongeza mjumbe huyo wa Bodi ya Wakurugenzi wa AGRA kwa uamuzi wake wa kutembelea mkoa wa Rukwa hatua itakayoongeza chachu kwa wakulima kuzalisha mazao .
Katika ziara hiyo, Rais mstaafu Kikwete amefuatana na Naibu Waziri wa Kilimo Anthony Mavunde pamoja na viongozi wa shirika la AGRA na Britten.
Mpui AMCOS ni wanufaika wa ufadhili unaotolewa na AGRA.
0 Comments