Header Ads Widget

MNEC ASAS AKEMEA MADALALI WA SIASA CHAGUZI ZA CCM

 


MJUMBE wa  halmashauri  kuu ya  chama  cha mapinduzi (NEC) Taifa anayewakilisha mkoa  wa  Iringa Salim  Abri  Asas amewataka  viongozi  wa CCM  kuwa makini na  madalali  wa  siasa  ambao wamekuwa  wakiibuka  kipindi cha chaguzi kwa  lengo la  kujipatia  fedha  kwa  viongozi  waliopo madarakani ama  wagombea.

Huku  akiwataka   wana  CCM kuelekea  chaguzi  za chama  kujiepusha na rushwa  kwani  iwapo  kila mmoja aliwajibika  wanachama  ndio  ambao  watatoa  kura na kama  kiongozi  hukuwajibika basi  subiri  hukumu badala ya  kufanya  siasa  za  kuchafuana.

Akifungua  kikao  cha maalum cha  Halmashauri  kuu ya  CCM wilaya ya  Iringa  vijijini katika  ukumbi  wa  Siasa ni  Kilimo juzi ,Asas  alisema  kuwa   madalali  hao  wa  siasa wamekuwa wakiibuka kipindi  cha chaguzi tu na miaka yote mine hawajapata  kuonekana  ila  sasa  wanakuja  wakijua kabisa wanaweza  kupata chochote kupitia siasa .

“ Ndugu   wajumbe kila    kiongozi  wa CCM alipewa dhamana ya  uongozi baada ya  kusimama jukwaani na kuahidi  kusimamia utekelezaji wa Ilani  ya CCM hivyo  kwa  wale  waliotimiza wajibu wao vizuri  madalali wa  siasa hawatakuwa na nafasi  ya  kuwarubuni  ila wale  ambao  hawakutimiza  wajibu  wao  ndio  watasikiliza maneno ya  fitina na chuki  kutoka kwa  madalali hao” alisema  Asas

Kuwa ni  vizuri  kila kiongozi  ndani ya  CCM mkoa  wa  Iringa  kujitathimini ametekeleza  vipi ilani ya  CCM na  yale  ambayo waliahidi  kwenye  chaguzi yametekelezwa ila  kabla ya  kuchukua  fomu ya  kuomba tena  nafasi  kuwa na majibu ya yale  uliyoahidi  jukwaani  wakati wa kuomba kura  vinginevyo  utahojiwa toka  umechaguliwa  ulikuwa  wapi na umefanya   nini  katika utekelezaji  wa ilani ya  CCM .

Katika  hatua  nyingine  Asas  alisema  jitihada kubwa   zilizofanywa na Rais Samia Suluhu  Hassan katika  ujenzi wa  vyumba  vya madarasa ni  kubwa na  kuwa  wao kama wana CCM na  watanzania wote wanajivunia sana  jitihada  hizo kwani leo shule   zinafunguliwa  kwa wanafunzi  wote  waliofaulu  kwenda  shule hakuna uhaba tena  wa  vyumba  vya madarasa  jambo  ambalo  ni la  kupongeza sana serikali . 

Alisema  miaka  mingine  kwa  kipindi  kama  hiki  wakuu wa wilaya  na wakuu  wa mikoa  pamoja na  watendaji wengine wa  serikali  wakiwemo  wakurugenzi  huwa wanakimbizana na  ujenzi wa vyumba vya madarasa  lakini kwa  mwaka  huu  hakuna  tena  kero  hiyo  na hata  wao kama wadau wa maendeleo  hakuna  barua  yoyote  ambayo  wamepokea   kuombwa  michango ya  ujenzi wa vyumba vya madarasa ama madawati .

“  Ninani hapa  amefuatwa   kuombwa  mchango  wa vyumba  vya madarasa  naona  hakuna hata  mmoja  sasa mnataka  mheshimiwa  Rais Samia atupatie nini hivi  ndio  anaanza   tujiandae  kwa mambo  makubwa na mazuri  mbele ya  safari pia  sisi  viongozi twendeni kwa  wananchi  tukayasemee haya yote”


Asas  alisema  kuwa utendaji kazi mzuri  wa Rais  Samia na serikali ya  awamu ya  sita  ndio  ambao  umepelekea  wao kama   viongozi  wa siasa  kutembea  kifua mbele.

Kwa upande  wake  Mbunge wa   jimbo la Kalenga Jackson Kiswaga  alisema  kuwa  pamoja na  ujenzi  wa  miradi ya elimu ,Rais   Samia  amesimamia  vema  ujenzi  wa miradi ya  barabara  ,maji na miradi  mingine  ambayo  imekuwa  mkombozi mkubwa kwa  wananchi  .

Hata   hivyo alishauri   wajumbe wa kikao   hicho  wanapompongeza Rais Samia wasisahau  kupongeza wabunge maana   wabunge  ndio  ambao  wanaomba  miradi  hiyo  bungeni na Rais ,mbunge na diwani  ni  wote  wanawajibika kuwatumikia wananchi na  wote  walichaguliwa  kutekeleza ilani ya  CCM .

Mwenyekiti  wa CCM wilaya ya  Iringa  vijijini Costantino Kihwele  aliwataka  watendaji  wa Halmashauri ya  Iringa  kuendelea kutekeleza  miradi mbali mbali kwa kasi waliyoanza nayo na  kuwa  wao kama  chama  wanavutiwa na  kasi ya  utendaji  wa  viongozi wa Halmashauri  hiyo .

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI