MWENYEKITI wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mussa Ndomba amesikitishwa na kitendo cha baadhi ya walimu wakuu kuorodhesha idadi kubwa ya uhaba wa vyumba vya madarasa ilhali vingine vimegeuzwa kuwa stoo za kuhifadhia madawati yaliyoharibika yanayohitaji ukarabati mdogo.
Ndomba ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea shule kongwe zilizopo kwenye Halmashauri ya Mji Kibaha ili kujua changamoto za shule hizo na kuzitafutia ufumbuzi.
Amesema kuwa jambo hilo lina changamoto kwani baadhi ya vyumba vya madarasa kufanywa stoo ya kuhifadhia madawati kwani endapo yangekarabatiwa ingeondoa changamoto kubwa ya uhaba wa vyumba hivyo.
Aidha amesema kuwa lengo kuzitambua ili wakati wa kupanga bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023 halmashauri kupitia idara ya mipango iweze kupanga namna ya kukabiliana na changamoto hizo.
Ameongeza kuwa amepita kwenye shule tano zenye jumla ya wanafunzi 7,456 na ameona kuwa kuna mahitaji mengi na kuitaka jamii ifanywe kwa kushirikiana na kamati za shule.
Katika ziara hiyo aliambatana na ofisa elimu ufundi Ramadhan Lawoga, ofisa Mipango Bashiru Ali kwenye shule hizo kongwe za Misugusugu iliyoanzishwa 1975, Kongowe1965, Miembe Saba1978, Kibaha 1958 na Msangani 1970.Halmashauri ya Mji Kibaha ina jumla ya Shule za Msingi 44 kati ya shule hizo, shule Kongwe ni 17.
0 Comments